• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Ni hatia kumsingizia mtu kuwa mchawi

Ni hatia kumsingizia mtu kuwa mchawi

Na WAANDISHI WETU

HUKU visa vya wazee kwa tuhuma za uchawi vikiendelea kukithiri haswa katika kaunti ya Kwale, Kilifi na Kisii, imebainika kuwa watu wanaotekeleza vitendo hivyo wanavunja sheria yenye adhabu kali.

Kulingana na sheria iliyopo sasa yeyote ambaye atapatikana na hatia ya kumsingizia mwenzake kuwa mchawi atatozwa faini ya Sh500,000 au asukumwe gerezani kwa miaka mitano, adhabu zote mbili.

Hii ni kulingana na Sheria za Kuhusu Uchawi sura ya 67 ambayo pia inaharamisha vitendo vya uchawi au ushirikina.

“Mtu yeyote ambaye atamtuhumu mwenzake kuwa mchawi au kuendesha shughuli za uchawi bila kutoa ithibati atakuwa ametenda kosa na atatozwa faini isiyozidi Sh500,000 au kifungo kisichozidi miaka mitano gerezani au adhabu zote mbili,” inasema sheria hiyo katika ibara yake ya sita.

Kulingana na sheria ni hatia kwa mtu kujifanya kuwa na nguvu za uchawi au ushirikina ambayo hutumia kuwasababishia watu wengine woga au majeruhi. Mtu kama atapewa adhabu ya miaka mitano gerezani.

Isitoshe, mtu kama huyo atahukumiwa kifungo cha miaka 10 gereza endapo atapatikana na hatia ya kushauri mtu mwingine jinsi ya kudhuru mwenzake au mali yake kuwa kutumia nguvu za uchawi.

Lakini licha ya kuwepo kwa sheria hii maafisa wa usalama hawajawashtaki watu wanaowaua wazee kwa tuhuma za uchawi.

Kwa mfano katika kaunti ya Kwale, jumla ya wazee 12 wameuawa kwa tuhuma za kuwa wachawi kuanzia Januari mwaka huu.

Akithibitisha visa hivyo, Kamishna wa Kaunti ya Kwale Josepha Kanyiri, Jumatatu alisema visa hivyo vimekithiri zaidi katika maeneo bunge ya Lunga Lunga na Kinango.

Aliongeza kuwa wazee wenye mvi na macho mekundu ndio hulengwa zaidi haswa na makundi ya vijana, wengine wakitoka familia zao.

“Uchunguzi wetu umebaini kuwa wazee wanaolengwa ni mwenye umri wa zaidi ya miaka 70 kwenda juu; wengi wakiwa ni wale ambao wamemea mvi. Inasikitisha kuwa mauaji hayo yanatekelezwa na watu wa familia za wahasiriwa,” akasema Bw Kanyiri.

Kamishna huyo alikariri kuwa ni kinyume cha sheria kwa mtu yeyote kumsingizia mzee kuwa mchawi au mshirikina akisema “kuota mvi au kuwa na macho mekundi sio ithibati kuwa mtu ni mchawi.”

Katika eneo bunge la Rabai, kaunti ya Kilifi Mzee Mwinga Lwambi Mwinga, 69, akishambuliwa na kuuawa Jumapili usiku na watu wasiojulikana kwa tuhuma za uchawi.

Kulingana na polisi, visa 67 vya mauaji ya wazee viliripotiwa mwaka uliopita na inahofiwa idadi itaongezeka mwaka huu.

Katika kaunti ya Kisii, wazee waliuawa mwishoni mwa wiki kwa madai ya kuwa wachawi.

Kulingana na kamishna wa kaunti ndogo ya Marani Patrick Murira, wanne hao wanawake watatu na mwanamume mmoja walidaiwa kumroga mwanafunzi mmoja ambaye ni mtahiniwa wa mtihani wa kidato cha nne (KCSE).

RIPOTI ZA: SIAGO CECE, MAUREEN ONGALA, WYCLIFFE NYABERI na CHARLES WASONGA

You can share this post!

Mwanachuo ashtakiwa kwa kutuma picha za ngono kwa mtoto wa...

Wanaotaka ugavana wamsuta Wetang’ula kupendekeza...

T L