JUSTUS OCHIENG’ Na SAMMY WAWERU
MUUNGANO wa Kenya Kwanza ulizindua Jumanne kikosi wa wawakilishi wake watakaoshiriki mazungumzo ya maelewano na upinzani.
Saba hao wanashirikisha Seneta wa Kakamega Dkt Boni Khalwale, Hillary Sigei (seneta Bomet), seneta maalum Essy Okenyuri, wabunge George Murugara (Tharaka), Mwengi Mutuse (Kibwezi Magharibi), Adan Keynan (Eldas), na Lydia Haika (mbunge mwakilishi wa wanawake Taita Taveta).
Wiki iliyopita, Azimio iliteua wawakilishi wake ili kufanya mazungumzo ya maelewano na serikali kuzima joto la kisiasa nchini.
Walioteuliwa na muungano huo unaoongozwa na aliyekuwa Waziri Mkuu Bw Raila Odinga wanajumuisha Katibu Mkuu wa Orange Democratic Movement (ODM) Edwin Sifuna, kiranja wa wachache seneti Ledama Ole Kina na naibu kiongozi wa wachache bunge la seneti Enoch Wambua.
Orodha hiyo pia inajumuisha wabunge Otiende Amollo (Rarieda), David P’Kosing (Pokot Kusini), Millie Odhiambo (Suba Kaskazini) na Amina Mnyanzi (Malindi).
Uteuzi wa wawakilishi wa pande zote, unajiri kufuatia ombi la Rais William Ruto kwa Azimio kusitisha maandamano nchini juma lililopita.
“Tuko tayari kwa mazungumzo ili kuleta amani nchini,” Dkt Ruto alisema, akirai upinzani kusitisha maandamano.
Bw Odinga aliongoza maandamano kadha, yaliyoshuhudia vurugu na kusababisha vifo vya watu kadha, majeraha na uharibifu wa mali na biashara Nairobi na Kisumu.
Kiongozi huyo wa ODM aliitikia ombi la Rais, ambapo anataka serikali kuangazia gharama ya juu ya maisha, sava ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kufunguliwa kubaini uhalisia wa aliyeshinda urais Agosti 9, 2022 na makamishna wa tume hiyo waliojiuzulu na kufutwa kazi kururejeshwa afisini.
Ruto hata hivyo anasisitiza matakwa ya Azimio, yanaweza kuangaziwa kupitia bunge.
Huku Kenya Kwanza ikidai Odinga anataka kushirikishwa serikalini, kiongozi huyo wa upinzani amepuuzilia mbali tetesi hizo akisisitiza kwamba nia yake kuona gharama ya maisha imeshushwa.
Amejitetea akisema hataki handisheki wala nusu mkate serikalini.