Na WINNIE ATIENO
WAWEKEZAJI wa sekta ya Utalii wamemlilia Waziri wa Utalii, Bw Najib Balala (pichani) kuwaokoa kutoka kwa sera zinazowakandamiza na kuathiri utalii.
Wakiongozwa na Mwenyekiti wa Muungano wa Utalii eneo la Pwani, Bw Victor Shitakha, walisema watalii wa kimataifa wanaendelea kuahirisha safari zao nchini kufuatia agizo la serikali la kutokubali wageni ambao hawajachanjwa, kuzuru sehemu za utalii ikiwemo mbuga za Wanyamapori na hoteli.
Wizara ya Afya ikiongozwa na Waziri Mutahi Kagwe na Bw Balala walitangaza kwamba kuanzia Disemba 21, ni sharti watalii waonyeshe thibitisho la kuchanjwa kabla ya kuruhusiwa kuingia sehemu za utalii hasa hoteli.
“Agizo hilo lilitangazwa wakati sekta ilikuwa ikinawiri na wageni wamejaa hoteli, hata hivyo waliokuwa wameanza kupanga safari walikatiza safari zao kutokana na sharti hilo. Licha ya hoteli kudinda kufuata masharti hayo makali waliweka mikakati ya kuhakikisha wanafuata masharti ya Covid-19,” alisema Bw Victor Shitakha mwenyekiti wa KCTA.