• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 3:31 PM
Ni roho mkononi maandamano yakiitikisa dunia

Ni roho mkononi maandamano yakiitikisa dunia

NA MASHIRIKA

NAIROBI, KENYA

NCHI tano duniani zinapanga kukabili maandamano ambayo yameitishwa na viongozi wa upinzani.

Nchi hizo ni Afrika Kusini, Kenya, Tunisia, Nigeria na Amerika.

Lengo kuu la maandamano hayo ni kuzielekezea shinikizo serikali hizo kwa changamoto za kiuchumi na kisiasa zinazoyakumba mataifa hayo.

Wadadisi wanasema huenda maandamano hayo yakawa ya kihistoria kote duniani, kwani yanafanyika kwa wakati mmoja.

Nchini Kenya, kiongozi wa upinzani, Raila Odinga, amekataa kile ametaja kuwa vitisho kutoka kwa serikali baada ya kutangaza leo Jumatatu kuwa siku ya maandamano kwa wafuasi wake.

Bw Odinga analalamikia gharama ya juu ya maisha na hali ya kutojali ya serikali kutokana na changamoto hizo. Ametaja maandamano hayo kuwa “makubwa zaidi” kuwahi kushuhudiwa Kenya.

Anasema kuwa maandamano hayo yanafuatia hatua ya Rais William Ruto kukataa kufunguliwa kwa seva za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kutokana na kile anadai kuwa “wizi wa kura” ulioendeshwa kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.

“Hatutakubali kutishwa na Rais Ruto na [Naibu Rais] Rigathi Gachagua. Ningetaka kuwaambia kwamba nilishiriki kwenye harakati za ukombozi wa pili wa nchi hii,” akasema Bw Odinga, aliyeshindwa kwenye uchaguzi wa urais mwaka 2022.

Nchini Amerika, aliyekuwa rais wa taifa hilo Donald Trump ameitisha maandamano ya wafuasi wake baada ya kueleza hofu kwamba huenda akakamatwa Jumanne.

Inadaiwa alimlipa mcheza sinema za ngono pesa ili kutotoa maelezo ya siri kumhusu.

“Habari za kijasusi zinaonyesha kuwa rais wa zamani wa Amerika atakamatwa Jumanne kwa makosa ambayo hakufanya,” akasema Trump kwenye ujumbe alioweka kwenye mitandao ya kijamii.

Hata hivyo, msemaji wake alisema kiongozi huyo hajafahamishwa rasmi kuhusu kukamatwa kwake.

Trump hajawasilisha ushahidi wowote kujitetea dhidi ya madai hayo.

Aliyekuwa Rais wa Amerika Donald Trump. PICHA | AFP

Mnamo Januari 6, 2021, wafuasi wa Trump walivamia majengo ya Bunge ya Capitol Hill kulalamikia kushindwa kwake kwenye uchaguzi mkuu wa Novemba 2020 na Rais Joe Biden wa Democratic.

Uchunguzi huo unajiri huku chama cha Republican kikijitayarisha kwa shughuli za uteuzi wa urais kwa uchaguzi mkuu wa 2024.

Nchini Afrika Kusini, Rais Cyril Ramaphosa alitoa onyo kali kwa kiongozi wa upinzani, Julius Malema, kabla ya maandamano makubwa yanayotarajiwa kuongozwa na chama chake cha Economic Freedom Fighters (EFF).

Kama nchini Kenya, maandamano hayo yamepangiwa kufanyika leo Jumatatu kwa ushirikiano na Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi nchini Afrika Kusini (SAFTU).

Nchini Tunisia, maandamano kama hayo yamepangiwa na upinzani kulalamikia gharama ya juu ya maisha, ukosefu wa usalama na ukiukaji wa sheria unaoendeshwa na serikali. Miungano mbalimbali ya kisiasa imekuwa ikimlaumu Rais Kais Saied kwa kushindwa kusuluhisha changamoto zinazolikumba taifa hilo.

Nchini Nigeria, upinzani umeandaa maandamano sambamba, ukilalamikia madai ya wizi wa kura kwenye uchaguzi uliofanyika mwezi Februari.

  • Tags

You can share this post!

Kalonzo akemea marafiki wanaopinga wito wa Azimio la Umoja...

TAHARIRI: Maandamano: Sheria ifuatwe

T L