NA PIUS MAUNDU
KINARA wa Wiper, Bw Kalonzo Musyoka amewakemea baadhi ya wandani wake ambao wanapinga maandamano yanayoandaliwa na upinzani leo Jumatatu.
Wafuasi wa Azimio la Umoja-One Kenya wanatarajiwa kushiriki maandamano ya kuelekea ikulu kushinikiza utawala wa Rais William Ruto ukabiliane na changamoto zinazokumba nchi na pia uondoke mamlakani.
Bw Musyoka amefichua kuwa anaunga mkono ‘maasi’ ya Bw Odinga dhidi ya serikali kwa kuwa hilo litamwongezea nafasi ya kuungwa mkono na waziri huyo mkuu wa zamani katika uchaguzi mkuu wa 2017.
Amewakemea baadhi ya wandani wake ambao hawataki kujiunga na maadamano ya leo Jumatatu na kuwataja kama watu “wenye tatizo la kiakili”.
“Watu hao wana tatizo la kiakili. Wanaona Raila ‘amejeruhiwa’ ilhali sasa wanamwekea makataa kwamba lazima aniunge mkono ndipo washiriki maandamano. Tunastahili kumuunga mkono sasa ili ikifika 2027 ashawishike kuwa tumetembea safari hii pamoja naye ili aniunge mkono. Lazima utata wote kuhusu uchaguzi wa 2022 usuluhishwe kabla ya kura ya 2027 kuzungumziwa,” akasema Bw Musyoka.
Makamu huyo wa rais wa zamani alikuwa akiwazungumzia wafuasi wake kupitia kituo cha redio cha Athiani akiwa ameandamana na Seneta wa Kitui Enoch Wambua na Mbunge wa Kathiani Robert Mbui.
Wanasiasa hao walisema maandamano ya sasa yataimarisha nafasi ya Bw Musyoka ya kuwania urais 2027 na kuungwa mkono na Bw Odinga.
Kati ya wandani wa Bw Musyoka ambao wamesema hadharani kuwa hawatashiriki maandamano hayo ni Gavana wa Makueni Mutula Kilonzo Jr, Seneta Daniel Maanzo na Gavana wa Machakos Wavinya Ndeti. Watatu hao wamekuwa wakimtaka Bw Odinga atangaze hadharani kuwa atamuunga Bw Musyoka.
Subscribe our newsletter to stay updated