NA MASHIRIKA
KYIV, UKRAINE
UKRAINE imeiomba Urusi kuandaa kikao cha “mazungumzo maalum” kuhusu mkakati wa kuwahamisha wapiganaji na raia waliokwama katika kiwanda kimoja cha kutengeneza chuma jijini Mariupol.
Ombi la Ukraine linafuatia kuibuka kwa video moja iliyoonyesha watu wakiwa wamejificha katika kiwanda cha kutengeneza chuma cha Azovstal, ambapo wanawake kadhaa walisikika wakisema walikuwa wamebakisha tu maji na chakula kitakachowasaidia kwa siku chache zijazo.
Inaaminika kuwa karibu raia 1,000 wa Ukraine wamejificha katika kiwanda hicho, Urusi inapojaribu kutwaa jiji hilo kutoka kwa udhibiti wa majeshi ya Ukraine.