Na LEONARD ONYANGO
KEMIKALI za plastiki zinazotumika kutengeneza vyombo vya kuhifadhi vyakula, vipodozi na vifaa vya watoto kuchezea (toys) zinachangia katika vifo vya mapema.
Ripoti ya utafiti uliofanywa nchini Amerika inasema kuwa vifaa hivyo vina kemikali inayojulikana kama phthalates ambayo ikiwa nyingi mwilini husababisha maradhi ya moyo.
Kemikali hizo hatari pia zinadumaza uzalishaji wa homoni na ubongo.
Tafiti za awali, zimewahi kuhusisha kemikali hizo na kutatizika kwa ukuaji wa sehemu nyeti za watoto wa kiume.
Aidha, tafiti zinasema kemikali hizo zinaweza kusababisha wanaume kuwa na mbegu hafifu, ugonjwa wa pumu (asthma), unene kupindukia (obesity), kansa na maradhi ya moyo.
Watafiti hao wanasema kuwa kemikali hizo huingia mwilini watu wanapokula vyakula vinavyohifadhiwa kwenye vifaa vya plastiki.
Watu 5,000 waliohusishwa katika utafiti huo walipatikana na kiwango cha juu cha kemikali hizo.
Watafiti hao walibaini kwamba watu walio na kiwango cha juu cha kemikali hizo wanakufa kabla ya kufikisha umri wa miaka 65.