• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 12:38 PM
Watu 26 wanaoishi na ulemavu Kiambu wapokea vifaa vya kazi kutoka NFDK

Watu 26 wanaoishi na ulemavu Kiambu wapokea vifaa vya kazi kutoka NFDK

Na LAWRENCE ONGARO

WALEMAVU wapatao 26 kutoka Kiambu, wamenufaika na vifaa vya kazi kutoka kwa mfuko wa Hazina ya Kitaifa Maalum kwa Watu Wanaoishi na Ulemavu (PLWDs) yaani National Fund for the Disabled of Kenya (NFDK).

Prof Julia Ojiambo, mmoja wa maafisa katika kamati ya hazina hiyo na naibu kamishna wa Thika Bw Mbogo Mathioya walihudhuria hafla hiyo.

Prof Ojiambo, alisema vifaa hivyo vya kazi kwa walemavu viligharimu takribani Sh650,000

Baadhi ya vifaa vilivyotolewa ni vya kutumika kwenye kinyozi, vifaa vya ususi, vifaa vya kazi ya useremala, cherehani za kushona nguo, na viti vya magurudumu.

Baadhi ya wanufaika wa mpango wa NFDK. Picha/ Lawrence Ongaro

Alieleza kuwa serikali imejitolea kuzunguka kote nchini kuona ya kwamba walemavu wanasaidiwa vilivyo.

“Tunatoa wito kwa walemavu popote walipo wajitokeza ili waweze kusaidiwa na serikali kupitia hazina hiyo,” alisema Prof Ojiambo.

Alitoa wito kwa walemavu popote walipo wajitokeze wazi ili serikali iweze kujali maslahi yao bila ubaguzi.

“Sisi kama wanakamata walio katika afisi ya hazina ya kusaidia walemavu tunafanya juu chini kuona ya kwamba hakuna mlemavu anabaguliwa Kwa vyovyote vile,” alifafanua Prof Ojiambo.

Alitaja baadhi ya shule ambazo wamesambaza misaada. Nazo ni Thika School for the Blind, Salvation Army, Thika JoyTown, na shule ya Maria Magdalena.

Bw David Muiruri ambaye ana ulemavu kwenye mguu wake wa kushoto, alisema azma yake imetimia kwa kupokea vifaa vya useremala.

“Ninaishukuru serikali kwa kufanya jambo la kupongezwa kwa kujali walemavu,” alisema Bw Muiruri.

Naibu kamishna Bw Mathioya aliwaonya walemavu hao wasiuze vifaa hivyo kwa manufaa yao wenyewe.

Mumepewa vifaa hivyo ili muzisaidie familia zenu, wala sio vya kuuza,” alionya afisa huyo wa wilaya.

Alisema mtu yeyote atakayepatikana ameuza vifaa hivyo atachukuliwa hatua ya kisheria.

“Tayari nimewaagiza machifu wangu wawe makini na kuhakikisha vifaa hivyo vinatumika ipasavyo,” alifafanua Bw Mathioya.

Aliwahimiza walemavu wazuru hospitali zilizo karibu nao, ili wapokee chanjo dhidi ya Covid-19.

Alisema wako katika hali hatari ya kuambukuzwa kulingana na hali yao ya kiafya na kwa hivyo wafanye hima.

Bi Purity Nguli ambaye alipokea cherehani ya kushona nguo, alipongeza serikali kwa kuwajali PLWDs.

Wanufaika waliohojiwa walisema hali yao ya maisha itabadilika kutokana na msaada ambao walipokea kutoka kwa serikali.

You can share this post!

KWA KIFUPI: Utakufa mapema ukihifadhi mlo kwenye vifaa vya...

Obado na watoto wake wanne kujibu mashtaka ya ufisadi wa...

T L