NA LAWRENCE ONGARO
WAFUGAJI wa ng’ombe wa maziwa wapatao 500 kutoka Gatundu walikongamana kwa mkutano wa hamasisho kuhusu ufugaji ambapo kampuni ya maziwa ya Brookside iliwapa mafunzo.
Walielimishwa kuhusu mbegu bora za kuzalisha ng’ombe wa maziwa kwa lengo la kuimarisha mapato.
Meneja mkuu wa maswala ya mifugo wa kampuni ya Brookside Bw Emmanuel Kabaki, alisema lengo lao kuu ni kusambazia wafugaji hao mbegu za ng’ombe wa gredi ili kuzitumia kupata mifugo ya ubora wa hali ya juu na maziwa mengi.
“Kampuni ya Brookside inalenga kuwahamasisha wafugaji wa ng’ombe, hasa katika Kaunti ya Kiambu ili waboreshe mapato yao yatokanayo na kuuza maziwa,” alisema Bw Kabaki.
Alitoa wito kwa wafugaji hao kuwa makini kwa kulisha mifugo yao nyasi ya kutosha ili wapate maziwa kwa wingi.
“Ni vyema pia wafugaji kuhakikisha mifugo inapumzika kwa saa 10 hadi 12 ili kutafuna nyasi kwa njia ifaayo,” alishauri meneja huyo.
Alisema wafugaji wanaopeleka maziwa yao katika kampuni ya Brookside hupata fedha zao kwa wakati bila kuchelewa.
Wakati wa hafla hiyo, mbegu 2,000 zilisambazwa kwa wafugaji hao. Kuna wataalam wa mifugo ambao watazuru makazi ya wafugaji hao ili kutekeleza shughuli ya upandikizaji wa mbegu.
Mwenyekiti wa wafugaji ng’ombe wapatao 1,300 wanaojitambulisha kama Gatundu United, Bw John Njau Gathanga, alisema wao huuza maziwa lita 10,000 kila siku.
“Tuna imani kuwa mbegu zitasaidia na kwamba tutapata ng’ombe wa kutoa maziwa maradufu,” alisema mwenyekiti huyo.
Alisema baada ya miaka miwili, watakuwa wamebadilisha ufugaji ili uwe wa kisasa.