NA MERCY KOSKEI
Mwanakontenti wa YouTube Diana Marua amepata nafasi ya 10 katika orodha ya wasanii wa kike walio na wasajili (subscribers) zaidi kwenye chaneli yao ya YouTube barani Afrika.
Utendaji wa kuvutia na bidii ya Diana ulimweka kama msanii wa kike wa pekee kutoka Kenya anayeongoza kwa walio na mitandao ya kijamii ya YouTube.
Kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook, WCB Wasafi walichapisha orodha iliyoonyesha kuwa mwanakontenti huyo ana wasajili 986,000.
Wanaoongoza katika orodha hiyo ni wasanii mashuhuri kama vile Zuchu kutoka Tanzania na wasajili 3 milioni, Yemi Alade wa Nigeria akiwa na wasajili 2.2 milioni akifuatwa na msanii maarufu wa injili Sinach akiwa na wasajili 2.1 milioni.
Wasanii wengine ni Eda Ehi, Ayra Starr, Tiwa Savage, Nandy, Rose Muhando, Guchi.
Mumewe Diana, Bahati alitumia mtandao wake wa kijamii ya Instagram kuelezea furaha yake na kumpongeza kwa mafanikio hayo muhimu.
Alistaajabia nafasi yake kwenye orodha hiyo, haswa ikizingatiwa kuwa ametoa nyimbo mbili pekee.
Katika chapisho lake, Bahati alikubali uingiliaji kati wa Mungu ambao umechangia mafanikio ya Diana.
“Angalia Mungu! Wengine wanashangaa kuhusu aina ya nyimbo anazoimba Diana. Mimi pia nashangaa… Ni Mungu! Hongera @Diana_Marua. Wasanii 10 wa Kike Waliosajiliwa Zaidi… No.1 nchini Kenya,” aliandika.