• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
CHOCHEO: Zidisha mashamsham, sizubae!

CHOCHEO: Zidisha mashamsham, sizubae!

Na BENSON MATHEKA

DELO alikuwa katika mkutano muhimu kazini mchumba wake Jane alipompigia simu.

Hakuweza kuijibu na akamtumia arafa kumweleza angempigia baada ya mkutano.

“Ok, switi, nakupenda sana,” Jane alijibu.

Baada ya mkutano, Delo alirudi katika ofisi yake na kumpigia Jane.

“Nilitaka kukuambia nakupenda sana mpenzi wangu,” Jane alimwambia.

Delo alihisi msisimko wa ajabu.

Akafurahi na kumjibu; “Switi, nakupenda zaidi.”

Uhusiano wa wawili hao umejengwa kwa kubadilishana jumbe na kutendeana mambo ya kudekezana jambo ambalo washauri wa masuala ya mapenzi wanasema ni muhimu sana kwa uhusiano wa kimapenzi.

“Shangaza mtu wako kwa mambo madogo. Usipofanya hivyo atakushangaa tu na kuchoka na uhusiano wenu. Mpigie simu na kwa sauti tamu ya upole umweleze unampenda na kumkosa. Kufanya hivi kunamchangamsha na kumfanya akuwaze kila wakati,” asema Titi Mueni, Mkurugenzi Mwandamizi wa kituo cha Big Hearts jijini Nairobi.

Titi asema makosa wanayofanya watu wengi ni kusahau wachumba wao wanapoondoka nyumbani kwenda kazini na kuwakumbuka wakiwaona jioni au wanapopata shida.

“Inashangaza watu hawakumbuki wachumba wao wakiachana asubuhi hadi wanapokutana jioni. Uhusiano wa aina hii ni sawa na ghorofa iliyojengwa kwenye changarawe. Inaweza kubomoka wakati wowote,” asema Titi.

Wataalamu wanasema kuwa hata kama mtu ana shughuli nyingi, anafaa kuwa akimshtua mchumba wake kwa ujumbe wa mapenzi mara kwa mara.

“Kukosa kumkumbuka mtu wako siku nzima kwa mwezi au mwaka kunaashiria hatari kubwa katika uhusiano wenu. Ikiwa haumkumbuki au kumuwaza asipokuwa karibu, kuna tatizo katika penzi lenu,” asema Francis Otiso mshauri wa wanandoa katika kituo cha Maisha Mema jijini Nairobi.

Kulingana na Otiso, hali hii inaashiria kuvunjika kwa mawasiliano jambo ambalo ni sumu kwa uhusiano wa mapenzi na ndoa.

“Uhusiano thabiti wa kimapenzi hujengwa kupitia mawasiliano bora. Yakikosa au kukatika huwa kuna hatari,” asema Otiso.

Vinette Wambui, mwanadada mwenye umri wa miaka 34, anasema kuwa aliokoa uhusiano wake wa kimapenzi kwa kuimarisha mawasiliano na mtu wake.

“Kuna demu aliyekuwa akimmezea mate mpenzi wangu. Nilipohisi hatari ya kupokonywa mpenzi wa roho yangu, nilijipanga, nikawa namtumia jumbe, maua, na kumpigia simu nikijua hana shughuli nyingi za kikazi. Hatimaye aliniposa tukafanya harusi,” asema Vinette.

Mwanadada huyu asema amedumisha mtindo huo hadi wakati huu, ikiwa ni mwaka wa sita katika ndoa.

Titi asema kuna watu wanaokosa kwa kusitisha waliyokuwa wakiwafanyia wapenzi wao kabla ya kuoana.

“Badala ya kusitisha uliyokuwa ukifanyia mtu wako kabla ya harusi, unafaa kuzidisha. Ikiwa anafanya kazi mbali na wewe, usilale bila kuwasiliana naye. Mrushie mabusu kwenye hewa na atalala akikuota ilivyokuwa alipokuwa akikurushia mistari,” asema Titi.

Mtaalamu huyu asema mawasiliano hayafai tu watu wakiwa mbali.

“Mtu wako akiwa nyumbani, usimpuuze uzame kwa mtandao. Mshirikishe kwa mambo anayopenda. Mpapase, mdekeze na umpikie mlo anaopenda. Ukifanya hivi utachota akili na roho yake na uhusiano wenu utakuwa imara,” aeleza Titi.

Kulingana na Otiso, mawasiliano ni moto unaoyeyusha matuta na matatizo yoyote yanayoweza kuibuka katika uhusiano wa kimapenzi.

“Tafiti kote ulimwenguni zimethibitisha kuwa mawasiliano yakisukwa vyema, ni tiba ya matatizo yanayovuruga mahusiano ya kimapenzi na kuvunja ndoa nyingi,” asema. Titi asema tatizo ni watu kuzoeana hasa baada ya kuoana.

“Shida ni kuwa watu wakiolewa au kuoa huwa wanahisi kuwa wamefika, wanamiliki wake na waume zao badala ya kupalilia uhusiano wao,” asema. “Kumiliki mtu wako ni kumuonyesha unamjali na hii ni kuimarisha mawasiliano,” aongeza.

You can share this post!

Kemsa lawamani tena hospitali zikikosa dawa

FUNGUKA: ‘Sitoi hata ndururu’