• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 10:55 AM
FATAKI: Komesheni tabia ya kutia mkono chunguni kabla mboga kuchemka

FATAKI: Komesheni tabia ya kutia mkono chunguni kabla mboga kuchemka

Na PAULINE ONGAJI

MAPEMA wiki hii nilikutana na chapisho fulani la kuchekesha kwenye mtandao mmojawapo wa kijamii.

Chapisho hilo la binti fulani liliandamana na picha iliyoonyesha vyakula vilivyopakiwa vizuri kwenye vifaa vya plastiki na kuwekwa kwenye friji.

Chini yake kulikuwa na maandishi… “kila wiki ninapomtembelea mpenzi wangu, lazima nihakikishe kuwa nampikia na kumhifadhia chakula cha kumtosha juma nzima…”

Ni picha iliyosababisha hisia mseto kutoka kwa wanamitandao. Hasa nakumbuka maoni fulani ya kudhihaki kutoka kwa binti fulani yaliyosema… “juma lililopita uliweka chumvi nyingi….”

Japo naamini kwamba ulikuwa utani, yaliakisi hali halisi ya yanayowakumba mabinti wanaojitoa kijasho kwa kuyashughulikia mahitaji ya madume ambao hawajawaoa wala kuwachumbia rasmi, wakidhani kwamba hayo ni mapenzi.

Hii yanikumbusha kisa cha kaka mmoja miaka kadhaa iliyopita aliyekuwa akinung’unika kwa sababu binti mmoja alikuwa “amevamia” nyumba yake na kutaga mayai.

Yaani kipusa huyo alikuwa amejileta nyumbani mwa kaka huyo na kwa wiki tatu mfululizo hakuwa anaonyesha dalili za kurejea alikotoka.

Naelezwa kwamba ni mojawapo ya sababu kuu ambazo zimewafanya akina kaka wengi siku hizi kuzembea inapowadia wakati wa kufuata utaratibu unaohitajika kabla ya kupata mke.

Nasikia kwamba madume siku hizi hufurahia kila wanapotembelewa na vipusa wikendi kwani wanajua watapiga deki, kuwapikia na kuwapa huduma nyingine muhimu bila malipo.

Dhana hii ni sababu tosha ya kuonyesha jinsi kuna baadhi ya mabinti wanaojishusha thamani wakidhani hii ni ishara ya mwanamke bomba.

Ya nini uchubue mikono yako ukimfulia na kumpikia kaka ambaye huna uhakika kwamba atakuoa?

Ya nini kumpa burudani na hata hajathibitisha uhusiano wenu?

Najua wanasema sehemu hiyo si sabuni eti itaisha lakini mbona kumpa mtu asiyestahili?

Ujumbe huu ni kwa wale warembo unaowapata kila wikendi wakiharibu kucha wakiwafulia madume huku wakijua sio wao pekee wamo mpangoni.

Kumbuka kuwa wengine hawapewi hata nauli. Nakumbuka binti mmoja akilalama jinsi baada ya wikendi zima akipiga deki na kumpa mahaba kaka, hata hela za P2 (kinga mimba) hakupata ng’o!

Japo wanayofanya baadhi ya madume hawa ni makosa, utawalaumu vipi?

Wengi wao hujiuliza, ya nini nimnunue ng’ombe ilhali ninaweza nikapata maziwa ya bure?

You can share this post!

UMBEA: Jinsi unavyoweza kuwasha moto hisia tena hadi...

Manchester City yalipiza kisasi dhidi ya Chelsea ligini