KIGODA CHA PWANI: Matarajio ya Wapwani kisiasa mwaka mpya unapoanza leo
PHILIP MUYANGA NA JURGEN NAMBEKA
MWAKA wa 2022 uliokamilika jana Jumamosi ulikuwa na mafanikio mengi kwa wanasiasa wa eneo la Pwani, wengi wao wakichaguliwa na kuteuliwa kutumikia Wakenya katika nyadhifa mbalimbali.
Kuanzia kwa Bw Amason Kingi, ambaye alichaguliwa kuwa spika wa bunge la seneti, hadi kwa Bi Aisha Jumwa aliyefanikiwa kuwa waziri wa huduma ya umma.
Mwaka ambao pia ulitishia umaarufu wa chama cha ODM katika eneo la Pwani. Kinara wa chama hicho Bw Raila Odinga, aliduwazwa na takwimu za uchaguzi wa Agosti 9, zilizoonyesha kuwa alimshinda rais Ruto katika kaunti ya Mombasa kwa asilimia 17 pekee.
Leta pamoja
Aidha ni mwaka uliowaleta pamoja viongozi wa Pwani baada ya uchaguzi, na kuibua minong’ono miongoni mwa wanasiasa hao kuwa kuna umuhimu wa kuungana kama Wapwani.
Licha ya kuwa pande tofauti za kisiasa, wanasiasa wa Pwani wameonekana wakifanya kazi kwa pamoja, ishara kuwa kuna uwezekano wa kutokea ushirikiano wa Wapwani kisiasa.
Kwa hakika orodha ya yaliyotendeka mnamo 2022, huenda yakianza kutajwa, tutakosa muda.
Ila hayo yakijiri, swali la kuulizwa ni: Je, mwaka 2022 umekamilika, tutarajie nini Mwaka Mpya 2023? Utabiri wa kisiasa unaonyesha huenda 2023 ukawa mwaka wa matukio makubwa ya kisiasa. Jambo ambalo wataalamu wa masuala ya siasa wamekubaliana nalo.
Kulingana na mshauri wa mauzo ya kisiasa Bw Bozo Jenje, kuna matarajio mengi katika mwaka huu mpya. Anaeleza kuwa kuna uwezekano wa wanasiasa kujipendekeza kwa serikali tawala. Hili ni pendekezo ambalo mtaalamu wa mawasiliano Ayub Mwangi, anakubaliana nalo. Kwa Bw Mwangi, upande wa upinzani bado unatapatapa na haujapata msingi thabiti wa kukaa nje ya serikali.
“Viongozi wengi ambao hawapo katika chama tawala bado wanatafuta pa kuelekea. Utakuwa mwaka wa kujitafuta kisiasa,” anasema Bw Mwangi.
Mahitaji yao
Kwa Bw Jenje, huenda muda mwingi wa wanasiasa wa ukanda wa Pwani ukatumika kushughulikia mahitaji yao na siyo wananchi.
“Mwaka huu utakuwa na mabadiliko mengi kwa maoni yangu. Badala ya viongozi kutilia maanani maendeleo na matatizo sugu ya wananchi, watachukua muda mwingi sana katika siasa za mageuzi ya kikatiba,” anahoji Bw Jenje.
Aidha, kwa kutetea maslahi yao, maendeleo muhimu ya wannachi wanaoongoza yatadorora pakubwa.
Mchambuzi wa siasa Bi Maimuna Mwidau anakubaliana na Mabw Jenje na Mwangi.
“Kila mwanasiasa atakuwa akitafuta muungano atakaoungana nao kutafuta nyadhifa mbalimbali. Walio na umaarufu watalazimika kuamua iwapo watajiunga na chama tawala UDA, na kutokuwa nje ya serikali.
Wengine pia watajiunga na miungano mingine ya kuwawezesha kutimiza malengo yao na siyo ya Pwani kama eneo,” anasema Bi Mwidau.Bi Mwidau anahoji pia kuwa, huenda siasa za Pwani zikabadilika zaidi. Kulingana naye, kuna uwezekano kuwa, kutazinduliwa chama kipya chenye chimbuko lake katika eneo la Pwani. Chama hiki kulingana naye kitalenga kuziba ufa ulioachwa na chama cha upinzani ODM, ambayo awali kilikuwa kimeshika ? Pwani na kuwa na wafuasi wengi.
Mvutano
“Kuundwa kwa chama kipya kutoka Pwani kitaleta mvutano. Mvutano huu baina ya chama cha Pamoja African Alliance(PAA) na chama hiki kipya kitaleta mgawanyiko katika kura za Pwani. Kitaishia kuzuia chama cha UDA, kupata kura zote za Pwani,” anahoji Bi Mwidau.
Kwa wachambuzi hawa wenye ufahamu mzuri wa siasa za ukanda wa Pwani, mwaka wa 2023 utakuwa nafasi murwa ya kaunti za Pwani kujiwezesha kiuchumi.
“Tunapoingia katika mwaka mpya, ni fursa nzuri ya viongozi wetu kutafuta kujiondoa katika kutegemea mataifa ya Dola kusuluhisha shida za hapa na pale. Ni wakati wa kusuluhisha matatizo yetu kama vile ukosefu wa chakula,” anasema Bw Jenje.
Mwaka mpya unapoanza hii leo, Wapwani wana imani kuwa viongozi wao watawafikiria wanapofanya maamuzi licha ya msemo mwanasiasa ni mwanasiasa.
Ni mwaka wa kuangalia karata ya siasa inavyochezwa na iwapo, itawafaidi wa Pwani au kuzidi kuwaacha katika njia panda kwa manufaa ya wanasiasa.
Next article
Ajenti ashtakiwa kwa kumtapeli mama mwenye mtoto anayeugua...