MPENDWA msomaji, leo tutagusia utanzu wa Semi.
Semi ni tungo fupi zinazowasilisha ujumbe kwa kufumba au kuchora picha ili kutoa ushauri kwa wanajamii. Pia huitwa tungo fupi.
VIPERA VYA SEMI
Misemo
Ni fungu la maneno machache linalobeba maana fiche. Hususan huunganisha dhana mbili kuwa moja? Mfano wa misemo:
i) Arusi ya mzofafa – arusi iliyojaa mbwembwe na madoido
ii) Macho ya chawa – kuwa na macho madogo
iii) Shilingi kwa ya pili – kufanana
Nahau
Ni utungo mfupi unaotumia maneno ya kawaida kuibua maana fiche. Huchukua muundo wa kitenzi pamoja na nomino; T + N = Nahau
Mifano
Shika sikio – kataza mtu kutenda mabaya
Tia shime – himiza mtu
Piga ramli – kubashiri/tabiri kama anavyofanya mganga
Misimu au simo
Ni maneno yanayozuka baina ya makundi ya watu wenye uhusiano wa karibu na hutumiwa kimafumbo kati yao pekee. Maneno hayo huzuka na kutoweka baada ya muda mfupi. Hata hivyo, yakidumu husanifishwa na kuwa msamiati wa kawaida wa lugha husika. Mifano ya misimu
Sonko – tajiri
Kufinywa – kudhulumiwa
Jisikia sukari – kuringa
Methali
Ni kauli za kimapokeo ambazo hufumba ujumbe/ushauri kwa njia ya mkato. Huwa na maana ya nje/bayana na maana ya ndani/batini. Mifano ya methali
(i) Mgomba changaraweni haupandwi ukamea
(ii) Lakabu Chiriku mzee hakamatwi kwa makapi
Vitendawili
Ni kauli fupi kwa njia ya maswali zenye maana fiche. Mifano ya vitendawili; Kitendawili? Tega!
i) Aliwa, yuala, ala na aliwa? – papa
ii) Kiti cha dhahabu hakikaliwi na watu? – moto
Shirikina
Tungo zinazobainisha imani tofauti za jamii husika. Kwa mfano; Ukila chakula gizani utakula na shetani.
Bundi akilia karibu na nyumba mtu mmoja wa nyumba ile atafariki. (maneno 305)
Mwandalizi: Mwalimu Borwo Chepkoit
Mkuu wa Idara ya Kiswahili
Shule ya Upili ya Wasichana ya Alliance