NA CHRIS ADUNGO
KATI ya masomo yote aliyoyafanya Dkt Alexander Rotich katika Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCE) mnamo 1983, Kiswahili ndicho kiliongoza.
Ingawa alipata nafasi ya kujiunga na Shule ya Upili ya Kabianga iliyoko Kaunti ya Kericho kwa minajili ya kiwango cha A-Levels, alihiari kusomea Shule ya Upili ya Tengecha (1984–1985).
Ilhamu yake ya kuchapukia Kiswahili ilichangiwa na baadhi ya wanafunzi waliowatangulia kimasomo shuleni Tengecha, akiwemo Prof John Habwe – mwandishi maarufu wa Isimu na Fasihi ya Kiswahili ambaye kwa sasa ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi.
Rotich alizaliwa Septemba 9, 1965 katika kata ya Kimuchul, eneo la Chemaner, Kaunti ya Bomet. Ndiye mwanambee katika familia ya watoto 18 wa Mzee Jonhstone Kiprotich Tuwei na wake zake wawili – Bi Rebecca Chebet na Bi Zipporah Tuwei.
Safari yake ya elimu ilipitia katika Shule ya Msingi ya Kimuchul (1972–1979) kisha Shule ya Upili ya Christ The King, Kaunti ya Nakuru (1980–1981) na Tengecha, Kericho (1982–1983).
Baada ya kukamilisha A-Levels, alipata kibarua cha kufundisha katika Shule ya Upili ya Chemaner mnamo 1986 kabla ya kuhamia katika Shule ya Upili ya Merigi, Bomet (1987–1988).
Alisomea ualimu baadaye katika Chuo cha Mafunzo ya Walimu cha Kisii (1989–1991) na Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) ikamtuma kufundisha katika Shule ya Upili ya St Michael’s Bomet. Alihudumu huko kwa kipindi kifupi kabla ya kuhamia katika Shule ya Upili ya Mulot, Bomet (1993-1996) kisha Shule ya Upili ya Chemaner (1996-1997).
Haja ya kujiendeleza kitaaluma ilimpa msukumo wa kujiunga na Chuo Kikuu cha Moi, Eldoret kusomea shahada ya kwanza katika ualimu (Kiswahili/Dini) kati ya 1998 na 2001.
Baada ya kuhitimu, TSC ilimtuma katika Shule ya Upili ya Kapsimbiri, Bomet. Alifundisha huko hadi 2005 kabla ya kurejea katika Chuo Kikuu cha Moi kusomea shahada ya uzamili huku akifundisha katika Chuo cha Mafunzo ya Walimu cha Mosoriot, Kaunti ya Nandi. Alifuzu 2009.
Rotich amewahi pia kuwa mhadhiri wa muda katika Chuo Kikuu cha Moi, Bewa la Kericho, alipokuwa mkufunzi katika Chuo cha Mafunzo ya Walimu cha Kericho (2008-2013).
Alianza kusomea shahada ya uzamifu (phD) katika Chuo Kikuu cha Moi mnamo 2010 na akaajiriwa na Chuo Kikuu cha Kabianga miaka mitatu baadaye kuwa Mhadhiri Msaidizi. Alifuzu 2018, mwaka mmoja kabla ya kupanda daraja kuwa Mhadhiri.
Kubwa katika maazimio yake kwa sasa ni kukwea zaidi ngazi ya elimu, kuwa Mhadhiri Mwandamizi na kuweka hai matumaini ya kuwa Profesa wa Kiswahili.
Uandishi ni sanaa iliyoanza kujikuza ndani ya Rotich akiwa mwanafunzi wa shule ya msingi. Insha nyingi alizoziandika wakati huo zilizomvunia tuzo za haiba kutoka kwa walimu wake. Alitunga pia mashairi ya kizalendo yaliyofana katika mashindano ya ngazi na viwango mbalimbali na kumpa fursa ya kupanda majukwaa tofauti ya makuzi ya Kiswahili.
Kufikia sasa, anajivunia kuchapishiwa makala kadhaa ya kitaaluma katika sura za vitabu na majarida mbalimbali ya kitaifa na kimataifa. Ameshiriki pia uandishi wa kitabu cha gredi ya tano katika lugha za Kikalenjin kwa minajili ya Mtaala wa Umilisi na Utendaji (CBC).
Tangu 2017, Dkt Rotich amekuwa Afisa wa Mahusiano Bora wa CHAKAMA–Kenya na yuko mstari wa mbele kuwalea wanachama wa Chama cha Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Kabianga (CHAKIKA) kwa ushirikiano na Dkt Mohamed Ramadhan Karama, Dkt Emmanuel Kisurulia na Prof Issa Mwamzandi.
Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki (CHAKAMA) na Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU) pia ni asasi ambazo zimempa majukwaa mwafaka ya kusambaza maarifa, kuendeleza msingi imara wa lugha na kutoa mchango mkubwa katika uandishi, utafiti na ufundishaji wa Kiswahili.
Dkt Rotich kwa sasa ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Usimamizi wa mojawapo ya shule katika Kaunti ya Bomet na ni mwanachama wa Bodi ya Usimamizi katika shule moja nyingine katika kaunti hiyo.
Anaistahi sana familia yake inayozidi kuiwekea kazi yake mshabaha na thamani.
Kwa pamoja na mkewe Bi Rachael Rotich, wamejaliwa watoto watatu – Winnie Chepkorir, Harriet Chepng’eno na Collins Kiplang’at.
Subscribe our newsletter to stay updated