NA CHRIS ADUNGO
TIMOTHY Kinoti M’Ngaruthi alizaliwa mnamo 1967 katika kijiji cha Kanthungu, Ruiri, Kaunti ya Meru.
Ndiye kitinda mimba katika familia ya watoto tisa wa marehemu Mzee M’Ngaruthi M’Kirigia na Mama Grace Kaguri.
Alisomea katika shule ya msingi ya Loire (1975-1983) na shule za upili za Chuka (1984-1987) na Kanyakine (1988-1989).
Ana Shahada ya Elimu (Kiswahili/Jiografia) kutoka Chuo Kikuu cha Egerton (1990-1994), Uzamili katika Kiswahili (Chuo Kikuu cha Kenyatta, 2008) na Uzamifu (PhD) kutoka Chuo Kikuu cha Chuka (2015).
Baada ya kuhitimu ualimu mnamo 1994, aliajiriwa na Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) na akapata fursa ya kufundisha katika shule ya upili ya Mataara, Thika (1994-1996), Kanjalu Girls, Meru (1996-1999) na Ruiri Girls, Meru (2000-2010).
Aidha, alikuwa mtahini wa kitaifa wa Fasihi ya Kiswahili na akawandaa wanafunzi wengi kwa ajili ya tamasha za uigizaji na uwasilishaji wa mashairi. Pia alikuwa mkaguzi katika tamasha mbalimbali, yakiwemo mashindano ya muziki na drama.
Dkt Kinoti amewahi kufundisha Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Kenya Methodist (KeMU) ambapo alikuwa Mkuu wa Idara ya Elimu (2015-2016) kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Embu mnamo Septemba 2016.
Amewahi kuwa mhadhiri wa muda katika Vyuo Vikuu vya Chuka, Mount Kenya (MKU), Tharaka na Meru.
Mbali na shughuli za kielimu, anasimamia maslahi ya wanafunzi wa kiume katika Chuo Kikuu cha Embu.
Amekuwa mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha za Kitamaduni chuoni humo, mwenyekiti wa Kamati ya Uhariri wa Miswada ya Sera, mhariri mkuu wa jarida la ‘Flashlight’ na mlezi wa Chama cha Kiswahili.
Kipaji cha uandishi kilianza kujikuza ndani yake akiwa mwanafunzi wa shule ya msingi. Alikuwa mwandishi stadi wa insha na mwigizaji mahiri.
Mazoea yake ya kusikiliza mashairi yaliyoghaniwa redioni na Abdalla Mwasimba (marehemu) yalimfanya mlumbi shupavu na mtunzi hodari wa kazi bunilizi.
Ari yake ya kukipenda Kiswahili iliongezeka mwaka wa 1987 alipopata fursa ya kushiriki kipindi Sanaa ya Kiswahili katika runinga ya VoK (sasa KBC).
Aliibuka bora zaidi kati ya washiriki wote na akawa maarufu miongoni mwa wanafunzi wenzake. Katika shule ya upili ya Kanyakine, alikuwa mwenyekiti wa Chama cha Kiswahili na katibu wa Chama cha Waandishi wa Habari.
Yeye na mwanafunzi mwenzake Kamau Munyua (Radio Citizen) walitambuliwa kuwa waandishi rasmi wa habari na kutengewa viti ndani ya basi kila mara timu za shule ziliposafiri kwa mashindano ya muziki, drama na michezo mingine.
Kufikia sasa, Dkt Kinoti amechapisha vitabu viwili, sura za vitabu na makala mengi katika majarida ya kimataifa na kuwasilisha makala mengi katika makongamano ya Kiswahili.
Pia ameandika hadithi fupi na hadithi za watoto ambazo anatarajia zichapishwe hivi karibuni. Vitabu vyake ni ‘Fasihi Simulizi na Utamaduni’ (JKF, 2008) kinachotumiwa na wanafunzi na walimu katika shule za upili na vyuo vikuu nchini na ughaibuni na ‘Miale ya Mashariki: Mashairi na Mwongozo wa Uchambuzi’ (Nsemia Inc. Ontario, 2012). Diwani hii yenye mashairi 82 imeidhinishwa na KICD kutumika katika shule za upili nchini Kenya.
Nje ya mazingira ya chuoni, Dkt Kinoti amewahi kuwa mlezi wa shule ya msingi ya Kanthungu na mwenyekiti wa Halmashauri ya shule ya upili ya Rwarera, Meru. Pia huhubiri neno la Mungu na kutoa ushauri nasaha katika makanisa na taasisi nyinginezo huku akiwa mfawidhi (MC) katika sherehe mbalimbali.
Anaitambua familia kama nguzo kuu ya ufanisi wake. Mkewe, Bi Hellen, binti zake Karwitha, Kajuju, Joy, Rehema na Belinda, pamoja na wajukuu wake humpa moyo wa kusonga mbele hata hali inapokuwa ngumu.
Subscribe our newsletter to stay updated