NA HASSAN MUCHAI
LEO tumebahatika kumpata mshairi, mhadhiri, mwanafalsafa , mtetezi wa dini na msomi maarufu kutoka taifa jirani la Tanzania.
Jina la Profesa Shabaan Yusuf Kibwana Nyagatwa Sengo au kama anavyojulikana na wengi kama Prof Tigiti Sengo si maarufu tu katika vyuo vyote vinavyotoa mafunzo ya lugha ya Kiswahili Afrika Mashariki ila pia nchi za Ulaya, Asia na kwingineko kote ambapo lugha hii inaenziwa.
Ingawa Prof Sengo amestaafu kazi ya uhadhiri, hafurahishwi na kauli aliyotoa Rais wa nchi ya Tanzania kuwahimiza raia wa nchi yake kukumbatia matumizi ya Kiingereza zaidi kuliko Kiswahili.
Anasema tangu 1965 amekuwa akifunza na kukilea Kiswahili na kwamba itakuwa vigumu sana kwa raia wa Tanzania kuafikiana na ombi la Mama Suluhu.
Wakati Taifa Leo ilipokutana naye na kumfanyia mahojiano hivi majuzi, iliajabia idadi kubwa ya wahadhiri mashuhuri wa kanda na kote ulimwenguni waliopitia mikononi mwake kupanua elimu yao au kutafuta shahada ya uzamili.
“Miongoni mwa wasomi wengi mashuhuri waliopitia mikononi mwangu ni Prof Kineene wa Mutiso, Prof Mugyabuso M Mulokozi, Prof D Masamba, Prof Said Ahmed, Mohammed Bakari, Prof Peter Mbaambu na wengine wengi ambao majina yao siwezi kuyakumbuka,” alisema wakati wa mahojiano na gazeti la Taifa Leo.
Ingawa Prof Sengo amestaafu kazi ya kuajiriwa, yeye huwasaili wanafunzi wanaotafuta shahada ya uzamili kote duniani.
Amekuwa akialikwa na kutoa mihadahara katika vyuo mbali mbali Afrika mashariki pamoja na taasisi nyingine zinazotoa mafunzo ya juu.
Prof Tigiti Sengo alizaliwa mwaka 1945 Kizuka, Ngerengere Kusini mwa Ngorongoro katika taifa la Tanzania ambalo wakati huo lilijulikana kama Tanga-Nyika (Tanga ikiwa na maana ya mji wa Tanga na Nyika pori). Alianza masomo yake mwaka 1956 katika shule ya msingi ya Kidugalo hadi darasa la nne kabla ya kuhamia shule ya msingi ya Ngerengere mwaka wa 1959.
Kati ya 1960 – 63 alikuwa Msamvu Middle School ambayo sasa ni chuo anwai cha Msamvu karibu na kituo kikuu cha Mabasi. Baada ya hapo, mwaka 1964 hadi 67 alikuwa katika shule ya upili ya Mzumbe kabla ya kujiunga na Dodoma Alliance 1968 – 1969 kwa mafunzo ya daraja la tano na la sita.
Baadaye alijiunga na chuo cha mafunzo ya kijeshi kwa muda wa miezi sita mnamo 1970 kabla ya mwaka huo huo hadi 1973 kupata mafunzo ya digrii ya ualimu kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam alikosomea lugha ya Kiswahili na Kiingereza.
Alibahatika kuajiriwa kama mhadhiri katika chuo hicho kazi aliyoifanya hadi kustaafu kwake mwaka wa 1996.
Kutokana na tajriba yake ya muda mrefu, Prof Sengo aliajiriwa na chuo kikuu cha Islamic University nchini Uganda hadi mwaka 2001 aliporudi nyumbani Tanzania na kuwa mhadhiri katika chuo huria cha Tanzania kama Profesa kabla ya kustaafu mwaka 2016. Kwa sasa anaishi mtaa wa Manzese, Dar es Salaam.
Ushairi
Kama walivyo washairi wengi, Prof Sengo alijiingiza kwenye fani ya ushairi kutokana na mvutio wa nyimbo za twaarab.
Anasema nyimbo za waimbaji kama vile Shakila Saidi wa Lucky Star, Juma Bhalloh zilimpunga. Alivutiwa zaidi na usomaji wa vitabu vya mashairi ya Shaban Roberts.
– Itaendelea Jumamosi ijayo.
Subscribe our newsletter to stay updated