• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 5:50 PM
NYOTA WA WIKI: Brennan Johnson

NYOTA WA WIKI: Brennan Johnson

NA GEOFFREY ANENE

BRENNAN ni mmoja wa mafundi wanaoongoza ufufuo wa washiriki wapya wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Nottingham Forest.

Chipukizi huyo, anayeweza kutumiwa kama kiungo mshambulizi ama winga, amekuwa mmoja wa mastaa wa EPL baada ya Kombe la Dunia 2022 kukamilika jijini Doha, Qatar, mwezi Desemba.

Amefunga mabao matano na kusuka pasi mbili zilizozalisha magoli kufikia sasa, fomu ambayo amekumbatia kama moto kichakani tangu kombe hilo kufika tamati.

Nottingham haijapoteza michuano mitano EPL tangu mwaka mpya uanze. Washirika hao wapya wa EPL waligawana alama na Chelsea katika sare ya 1-1 mwaka mpya Januari 1.

Wakazaba Southampton 1-0 siku tatu baadaye kabla kuingiza Leicester mitini kwa kuwachabanga 2-0 Jumamosi ya Januari 14.

Masogora hao wa kocha Steve Cooper kisha walilazimisha Bournemouth sare ya 2-2 Jumamosi iliyofuata na kufinya Leeds 1-0mnamo Jumapili iliyopita.

Bao la Brennan la hivi punde – la tano EPL – lilikuwa dhidi ya Leeds, licha ya kwamba anashiriki msimu wake wa kwanza kabisa katika Ligi Kuu.

Chipukizi huyu ana jumla ya magoli saba katika mechi 27 za mashindano yote nchini Uingereza msimu huu.

Isitoshe, alichangia pakubwa Nottingham Forest kupanda ngazi EPL kwa mara ya kwanza kabisa katika miaka 23, akiibuka mfungaji wao bora msimu uliopita.

Alitinga mabao 18 katika ligi ya daraja la pili Championship, mabingwa hao wa EPL mwaka 1978 na Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) 1979 na 1980 wakizinduka kutoka usingizini na kurejea Ligi Kuu msimu huu wa 2022-2023.

Tangu aanze soka akiwa na miaka minane, Brennan amesakatia Nottingham Forest pekee. Isipokuwa alikoanzia soka yake Dunkirk na wakati alipelekwa Lincoln City katika ligi ya daraja la tatu msimu 2020-2021.

Alichezeshwa sana na kuimarika kimchezo akiwa Lincoln; alifunga jumla ya mabao 13 na kumega pasi 14 zilizozalisha magoli, katika mechi 49.

Takwimu hizo zinadhihirisha kuwa mwana huyo wa mshambulizi wa zamani wa Bury, Ipswich Town na Nottingham Forest, David Johnson, anaweza kufanya makubwa hata zaidi msimu huu na ijayo.

Kimataifa, Brennan aliruhusiwa kuwakilisha mojawapo ya Uingereza alikozaliwa, Jamaica anakotoka babake ama Wales alikozaliwa mamake.

Alichagua Wales mwaka 2018 baada ya kuchezea timu ya Uingereza ya makinda wasiozidi miaka 17.

Alikuwa katika kikosi cha Wales kilichoshiriki Kombe la Dunia lililokamilika Qatar majuzi.

Chipukizi huyo anaaminika ndiye atafuata mshambulizi wa zamani wa Tottenham na Real Madrid, Gareth Bale, ambaye alistaafu soka ya kimataifa mwezi Januari.

  • Tags

You can share this post!

MALENGA WA WIKI: Zamu leo ni ya msomi maarufu na mshairi...

GUMZO: Auba hana raha tena Chelsea baada ya kutemwa UEFA

T L