• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Mikakati ya UhuRaila kutuliza mlima

Mikakati ya UhuRaila kutuliza mlima

Na WANDERI KAMAU

RAIS Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM, Raila Odinga, sasa wameanza juhudi mpya kutuliza joto la kisiasa katika ukanda wa Mlima Kenya ili “kuitengenezea mapito” ripoti ya Jopokazi la Maridhiano (BBI).

Hili ni baada ya kubaini kuwa idadi kubwa ya wenyeji bado hawajaikumbatia ripoti hiyo kikamilifu, hali inayotajwa na baadhi ya waandani wa Rais Kenyatta “kuzua wasiwasi miongoni mwao na rais mwenyewe.”

Hatua hiyo pia inaelezwa kuchangiwa na ripoti za kijasusi kuwa juhudi za serikali kuwatumia maafisa wa utawala wa mikoa kama machifu kujaribu kuipigia debe ripoti vile vile hazijazaa matunda.

Tayari, baadhi ya wanasiasa waliokuwa wakiipigia debe ripoti wamekimya kabisa huku tetesi zikiibuka kuhusu migawanyiko, usaliti na ushindani katika makundi ya kisiasa ya ‘Kieleweke’ na ‘Embrace.’

Makundi hayo ndiyo yamekuwa yakiandaa mikutano katika maeneo mbalimbali ukanda huo kuipigia debe.

Baada ya barua ya Seneta Irungu Kang’ata wa Murang’a kwa Rais Kenyatta kuhusu ugumu wa kuiuza BBI Mlimani, viongozi wengi wanazidi kujitokeza, miongoni mwao akiwemo Gavana Anne Waiguru wa Kirinyaga.

Kwenye mahojiano wiki hii, Bi Waiguru alionya kuwa huenda mchakato huo ukasam- baratika ikiwa viongozi hawatazingatia umo- ja na kutilia maanani malalamishi ambayo yametolewa na wenyeji.

“Ningetaka kuwashauri wale wanaoende- sha mchakato huu kufahamu kuwa hili ni suala la kisiasa. Lazima pawe na mazingira ya kusikilizana na kuwashirikisha viongozi wote hata ikiwa wana maoni au misimamo tofauti. Ikiwa masuala hayo hayatazingatiwa, basi kuna hatari kubwa juhudi zetu zisifaulu,” akaonya Bi Waiguru.

Duru zinasema hatua hiyo ndiyo ilimfanya Rais Kenyatta kubaini hali si shwari katika ngome yake, na kuamua kuchukua jukumu hilo yeye binafsi.

Inaelezwa uhalisia huo ndio ulimfanya Rais Kenyatta kufanya mahojiano ya pamoja na vituo vya redio vinavyotangaza kwa lugha ya Gikuyu mnamo Jumapili. Kwenye hotuba yake ambayo ilipeperush- wa Jumatatu, Rais Kenyatta aliwarai wenyeji “kunyakua kilicho chao kwanza” kwenye ripoti, badala ya kupewa ahadi ambazo hawajui watatimiziwa lini na wale wanaoipinga.

“Sisi (Mlima Kenya) ndio tutakaonufaika zaidi ikiwa Wakenya wataipitisha ripoti. Huu si mpango wa kumfanyia kampeni ndugu yangu [Raila] kama mnavyoambiwa. Je, Raila ana makao yoyote eneo hili? Acheni kupotoshwa na watu wanaoeneza uwongo,” akasisitiza Rais.

Rais pia alimlaumu vikali Naibu Rais Wil- liam Ruto na kundi la ‘Tangatanga’ akisema hawana sababu zozote maalum kuipinga ripo- ti.

“Hii ni safari ambayo tayari nimeianza na hakuna yeyote ambaye atanizuia kufika ninakotaka,” akaeleza. Wandani wake wa karibu walisema hatua yake kutumia vituo vya redio vya Kameme, In- ooro, Coro na Gukena FM kwa pamoja ilikuwa kuhakikisha ujumbe wake umewafikia watu wengi zaidi.

“Huo ulikuwa mwanzo tu. Rais ataanza kampeni kali kuwafikia wenyeji katika mae- neo ya mashinani ili kujaribu kupunguza uasi uliopo dhidi ya BBI,” akaeleza mshirika mmo- ja wa karibu.

Wadadisi wanasema Rais Kenyatta anaon- ekana kushirikiana na Bw Odinga kwenye juhudi hizo kwani tayari, (Odinga) ameanza kufanya vikao na makundi mbalimbali kuto- ka ukanda huo kama wazee, vijana na akina mama.

Kwenye vikao hivyo, Bw Odinga amekuwa akiwarai wenyeji kuwafikia wenzao kwenye maeneo wanakotoka ili kuhakikisha “ujumbe kuhusu manufaa ya ripoti hiyo unawafikia watu wengi zaidi.”

Mapema wiki hii, Bw Odinga alikutana na ujumbe maalum wa wazee wa jamii ya Agikuyu ulioongozwa na mwenyekiti wa Baraza la Wazee la jamii hiyo (KCA) Bw Wachira Kia- go katika eneo la Ruaka, Kaunti ya Kiambu. Bw Odinga pia alikutana na wafanyabi- ashara kutoka mtaa wa Githurai (Kiambu) ambapo pia aliwaomba kuiunga mkono ripoti.

Kwa mujibu wa wadadisi wa kisiasa, mbinu hizo mpya za Rais Kenyatta na Bw Odinga zi- nalenga kuhakikisha kuwa wametumia “njia tulivu” kushusha uasi huo.

“Rais Kenyatta hana lingine ila kuhakikisha ngome yake imeiunga mkono ripoti hiyo, kwani Bw Odinga amefanikiwa kudhibiti hali miongoni mwa wafuasi wake. Haina pingam- izi zozote miongoni mwao,” asema Bw Javas Bigambo, ambaye ni mdadisi wa siasa.

Kulingana naye, litakuwa pigo kubwa kwa Rais Kenyatta ikiwa Mlima Kenya itakosa kuunga mkono ripoti, hata ikiwa Wakenya wengine wataipitisha.

“Itakuwa ishara Rais amepoteza udhibiti na ushawishi wa kisiasa miongoni mwa wafuasi wake,” akaongeza Bw Bigambo.

Hata hivyo, Prof Macharia Munene, ambaye pia ni mchanganuzi wa siasa, anasema ingali mapema kudai kwamba Rais Kenyatta ame- poteza usemi wake eneo hilo. Anasema sababu kuu ni kuwa kampeni ras- mi za BBI bado hazijaanza.

“Ilivyo sasa, Rais Kenyatta bado ndiye mse- maji na kiongozi rasmi wa kisiasa Mlima Ken- ya. Hii ni licha ya mirengo tofauti ya kisiasa ambayo inaendelea kujitokeza. Hali halisi ita- julikana kampeni hizo zitakapoanza,” akasema Prof Munene.

You can share this post!

Kenya yasifiwa kutumia teknolojia kuzuia kuenea kwa corona...

Viongozi wataka Jaji Mkuu mpya ateuliwe kwa uwazi