Na CHARLES WASONGA
MUUNGANO wa Azimio la Umoja-One Kenya umepata pigo jingine baada ya wabunge 10 wa Jubilee kutoka Mlima Kenya kuamua kushirikiana na Kenya Kwanza “kuvutia maendeleo kwa watu wetu.”
Wakiongozwa na mkurugenzi wa uchaguzi katika chama hicho, Kanini Kega, wabunge hao walikutana na Naibu Rais Rigathi Gachagua mnamo Ijumaa.
Bw Kega, ambaye ni mbunge wa zamani wa Kieni ni mmoja wa wawakilishi tisa wa Kenya katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA).
Jubilee ni kimojawapo cha vyama tanzu katika muungano wa Azimio na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta bado ndiye kiongozi wake.
Hata hivyo, duru zinasema kuwa atajiuzulu wadhifa huo katikati mwa Februari sawa na cheo chake kama mwenyekiti wa Baraza Kuu la Azimio.
Japo, Bw Gachagua alisema ajenda kuu ya mkutano huo, uliofanyika afisini mwake, Jumba la Harambee House Annex, Nairobi, duru zimeiambia safu hii kwamba mada za kisiasa pia zilipewa kipaumbele.
Naibu Rais amekuwa mbioni kujikuza na kudhibiti siasa za Mlima Kenya ili atawazwa kuwa kinara wa eneo hilo lenye zaidi ya kura milioni nne (4 milioni).
Anapania kurithi wadhifa ambao umeshikiliwa na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta tangu 2013, baada ya kustaafa wa Hayati Rais Mwai Kibaki.
“Leo (Ijumaa), niliwakaribisha Wabunge kutoka Jubilee, chama chetu cha zamani, katika Harambee House Annex. Tulijadili masuala yanayohusiana na maendeleo katika maeneo wanayowakilisha,” akasema Bw Gachagua kupitia akaunti yake ya Twitter.
“Uchaguzi umeisha, na sharti tufanye kazi pamoja bila kujali miegemeo yetu ya kisiasa. Kwa hakika, Mheshimiwa Rais William Ruto na mimi tumekubaliana kwamba 2023 ni mwaka wa kazi, na sharti tuweke masilahi ya watu mbele kwanza ili kujenga upya uchumi wetu,” akaongeza.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa Mbunge Maalum Sabina Chege, ambaye pamoja na Bw Kega walioongoza kampeni za urais za kinara wa Azimio Raila Odinga katika eneo la Mlima Kenya, kuelekea uchaguzi mkuu uliopita.
Wengine waliokuwepo ni wabunge; David Kiaraho (Ol Kalou) Irene Njoki (Bahati), Zachary Kwenya (Kinangop), Dkt Shadrack Mwiti (Imenti Kusini ), Mark Mwenje (Embakasi Magharibi), Amos Mwago (Starehe), Dan Karitho (Igembe ya Kati), Stanley Muthama (Lamu Magharibi) na Seneta wa Lamu Joseph Githuku.
Ingawa mkutano huo ulisemekana kati ya Bw Gachagua na wabunge wa chama cha Jubilee, ambacho ni chama tanzu katika muungano wa Azimio wabunge wa chama hicho kutoka maeneo yaliyoko nje ya Mlima Kenya hawakuwepo.
Wao ni pamoja na Mbunge wa Sirisia John Waluke na mwenzake wa Eldas Aden Keynan, miongoni mwa wengine.
Hii ndio maana wadadisi wanasema kuwa suala kuu katika mkutano huo lilikuwa siasa za Mlima Kenya na ndoto ya Bw Gachagua la kumrithi Bw Kenyatta kama msemaji wa Mlima Kenya.
“Haja kubwa ya Bw Gachagua ni kumaliza kabisa Azimio na Jubilee katika Mlima Kenya ili kugeuza eneo hilo kuwa ngome ya Chama cha United Democratic Alliance (UDA) asilimia 100. Hili litamwezesha sio tu kuwa msemaji wa eneo hilo, bali pia kujiandaa kwa ajil ya kumrithi Rais Ruto atakapokamilisha muhula wake wa pili 2032,” anasema Dkt Reuben Nasibo, ambaye ni mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.
“Endapo Bw Gachagua atafaulu kuunganisha eneo la Mlima Kenya kisiasa na kushawishi wabunge hao wa Jubilee kuunga mkono Kenya Kwanza, Azimio itasalia jibwa lisilong’ata ndani na nje ya bunge,” anaongeza.
Lakini Bw Kega aliambia safu hii kwamba hatua yake na wenzake kukutana na Bw Gachagua haimaanishi kuwa wamegura Jubilee na kujiunga na Kenya Kwanza au UDA.
“Wakati huu mimi na wenzangu tungali wanachama wa Jubilee. Alivyosema Mheshimiwa Naibu Rais mada kuu wa mkutano wetu ulikuwa ni maendeleo,” akasema.
Akaongeza: “Juzi si uliona kinara wetu Raila akiwashauri magavana wa Azimio kushirikiana na serikali ili kufanikisha maendeleo katika kaunti zao. Na wiki jana, wabunge na viongozi wote wa Luo Nyanza walitangaza, wakati wa ziara za Rais eneo hilo, kwamba watafanyakazi na serikali katika nyanja ya maendeleo.”
Subscribe our newsletter to stay updated