NA MAGALENE WANJA
MKENYA Bosco Somi alikuwa na ndoto ya kuwa mwanamuziki tangu utotoni ila ndoto hiyo ilitoweka baada ya kugundua kwamba sauti yake haingemfaa kwa tasnia hiyo.
Kwa jinsi anavyopenda sana kutagusana na watu, kazi yake ya kwanza ilikuwa katika sekta ya mauzo ambapo anasema ilimsaidia yeye kujifunza mengi.
Kwa wakati mmoja, Bw Somi aliajiruwa kama msimamizi wa mauzo katika kampuni ya Roto Tanks ambayo ilikuwa inashirikiana na benki ya Equity kwa muda wa miaka 10.
“Katika miaka hiyo niliyoajiriwa, nilijifunza mengi kuhusu jinsi ambavyo ninaweza kuongeza mauzo na kuwavutia wateja katika biashara,” anasema Bw Somi.
Mambo hayakumwendea vizuri na kuna wakati alipoteza kazi yake na akashindwa jinsi ambavyo angeweza kuendelea na maisha yake bila mapato.
Mnamo mwaka 2013 alianzisha kampuni ya Sky Digitals, akiwa na nia ya kutoa suluhu kwa watu wenye ulemavu pamoja na vijana kupata huduma za mtandao kwa bei nafuu.
Alikuna kichwa na akabuni mtambo unaofahamika kama Wi-Fi Vending Machine.
“Kifaa hiki hufanya kazi kama simu za kitambo ambazo zilitumika kwa kuwekwa sarafu ili kuwezesha mawasilino,” anaeleza Bw Some.
Unapobonyeza alama ya Wi-Fi kwenye kifaa hicho, kiungo kinatumwa kwenye simu, kompyuta au kifaa cha kielektroniki na unaweza kutumia huduma ya mtandao.
“Unapopewa chaguo la “Insert coin”, unahitajika kuweka sarafu ya Sh10 au Sh20, ambayo inajionyesha kwenye kifaa hicho na dakika ambazo utaweza kutumia mtandao,” anasimulia Bw Somi wakati Taifa Leo ilitaka kufahamu namna mtambo huo unavyofanya kazi.
Mojawapo ya manufaa makuu ya mtambo huo ni kuwa unaweza kuunganisha vifaa 4,000 kwa wakati mmoja bila kuathiri utendakazi wake.
Manufaa mengine ni kuwa kwa kutumia mtambo huo, unaweza kutumia kiasi cha chini cha pesa kuanzia Sh10.