• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:50 AM
Ni mzaha tu, mke wa Samidoh si mjamzito

Ni mzaha tu, mke wa Samidoh si mjamzito

Na SAMMY WAWERU

MKE wa mwanamuziki wa nyimbo za Mugithi Samuel Muchoki maarufu kama Samidoh, Edday Nderitu Alhamisi usiku alitangaza kuwa na ‘ujauzito’.

Edday alitoa tangazo hilo kupitia ukurasa wake rasmi wa Facebook.

“Ni kiumbe mwenye nguvu zaidi kuwa ndani yako akikua. Hakuna zawadi kubwa kuliko hii. Si jingine ila ni maombi,” aliandika.

Chapisho hilo aidha liliandamana na picha, anayoonekana akiwa mwingi wa tabasamu.

Amevalia rinda maridadi, huku akiwa amepakata ujauzito.

Hana ujauzito

Hata hivyo, kupitia mmoja wa wandani wake katika mahojiano ya kipekee na Taifa Leo Dijitali imebainika tangazo hilo ni la utani tu.

Edday si mjamzito, mjuzi wetu aliarifu.

“Hana ujauzito, ni mzaha tu,” alisema, akiomba kubana majina yake.

Chapisho hilo lilijiri siku chache baada ya seneta maalum Karen Nyamu kufichua video akiwa pamoja na Samidoh, wakionekana kuzama kwenye lindi la mapenzi.

Video hiyo aidha imezua hisia mseto mitandaoni, hata ingawa Edday hazaizungumzia.

Licha ya msanii huyo kuwa na mke na watoto watatu, amekuwa kwenye uhusiano haramu na Karen hatua ambayo imekuwa ikimkosesha usingizi Edday.

Mapema mwaka huu, Edday alielezea masikitiko yake kufuatia uhusiano wa pembeni wa mumewe na seneta huyo akiapa kwamba hatakubali kuwa kwenye ndoa yenye zaidi ya mke mmoja.

Samidoh na Karen wana watoto wawili pamoja.

Huenda picha aliyopakia Edday, ya ujauzito, ni ya kitambo akitumia hatua hiyo kumjibu Karen kutokana na video ya majuzi.

Siku kadha zilizopita, Samidoh na mkewe walikuwa wamezuru Nyandarua kusambaza chakula cha msaada kupitia wakfu wake wa Guitar ya Samidoh Initiative.

Taifa Leo Dijitali imearifiwa kwamba Samidoh hakufurahia ufichuzi wa video hiyo, ikisemekana wawili hao sasa hawapatani.

Mwimbaji huyo ambaye pia ni askari, hata hivyo, hazaizungumzia.

  • Tags

You can share this post!

Mabaki ya wahanga 587 wa mauaji ya kimbari yafukuliwa...

Kivumbi kikali KWPL ikiingia raundi ya 17

T L