• Nairobi
  • Last Updated May 10th, 2024 1:50 PM
TAHARIRI: Mauaji ya kiholela ya wazee yakomeshwe

TAHARIRI: Mauaji ya kiholela ya wazee yakomeshwe

KITENGO CHA UHARIRI

INASIKITISHA sana kwamba visa vya mauaji ya kiholela ya wazee vinaendelea nchini bila hatua kali kuchukuliwa dhidi ya washukiwa.

Kisa cha hivi punde ni mauaji ya watu wanne katika Kaunti ya Kisii kwa tuhuma kwamba walikuwa wachawi. Visa kama hiki vimewahi kushuhudiwa awali katika maeneo kama vile Nyamira, Kwale na Kilifi.

Cha kushangaza ni jinsi makundi ya watu hujitokeza tu na kuchukua sheria mikononi na hatimaye hawachukuliwi hatua zozote na vyombo vya dola.

Kutochukuliwa kwa hatua kumewapa ujasiri wahusika kuendeleza mauaji zaidi.

Uchunguzi katika vingi vya visa hivi umeonesha kwamba wauaji huwa na sababu fiche za kuendeleza unyama huu na badala yake uchawi hutumiwa tu kama kisingizio.

Mathalan, uhasama baina na koo pamoja na tofauti nyinginezo za kijamii ndizo huwa baadhi ya vyanzo vya mauaji haya.

Kwa mfano kumewahi kuripotiwa hali ambapo vijana huwasingizia wazee wao kuwa wachawi na kushiriki katika mauaji yao kisha wawanie mali ya urithi.

Katika kaunti ya Kwale, walengwa huwa ni wazee wenye mvi na macho mekundu.

Jamii pana haifai kunyamazia ukatili huu.

Kimya cha jamii pamoja na asasi za serikali ndicho kichocheo cha mauaji zaidi. hatua za dharura zinafaa kuchukuliwa kukomesha uhayawani huu.

Inasikitisha hata zaidi kubaini kwamba ipo sheria inayoweza kutumiwa kukabili tuhuma za uchawi au ushirikina.

Kwa mujibu wa Sheria Kuhusu Uchawi sura ya 67, ni hatia kwa mtu kujifanya kuwa na nguvu za uchawi au ushirikina, hali inayotumiwa kuwasababishia watu wengine woga au majeraha.

Mtu kama huyo atapewa adhabu ya miaka mitano gerezani. Mtu kama huyo atahukumiwa kifungo cha miaka 10 gerezani endapo atapatikana na hatia ya kumwelekeza mtu mwingine jinsi ya kudhuru mwenzake au mali yake kwa kutumia nguvu za uchawi.

Kwa upande mwingine, sheria iyo hiyo pia inasema kwamba mtu yeyote ambaye atapatikana na hatia ya kumsingizia mwenzake kuwa mchawi atatozwa faini ya Sh500,000 au asukumwe gerezani kwa miaka mitano, au adhabu zote mbili.

Maadamu sheria ya kukabili uchawi au ushirikina ipo na vile vile sheria hiyo pia inaeleza hatua ambazo wanaowatuhumu wengine kuwa wachawi ipo, ina maana kwamba polisi na jamii pana ndiyo inazembea na hivyo kuchochea mauaji ya wazee katika jamii.

You can share this post!

Kibicho aonya wahuni wanaopanga kusambaratisha sherehe za...

Arsenal na Palace watoshana nguvu katika gozi la EPL ugani...

T L