• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Arsenal na Palace watoshana nguvu katika gozi la EPL ugani Emirates

Arsenal na Palace watoshana nguvu katika gozi la EPL ugani Emirates

Na MASHIRIKA

KOCHA Patrick Vieira amesema bao la sekunde za mwisho ambalo Arsenal walifunga dhidi ya kikosi chake cha Crystal Palace katika sare ya 2-2 mnamo Jumatatu usiku ugani Emirates lilimsikitisha zaidi.

Fowadi Alexandre Lacazette alitokea benchi katika kipindi cha pili na kunyima Palace ushindi muhimu dhidi ya Arsenal waliotangulia kufunga kupitia nahodha Pierre-Emerick Aubameyang.

Chini ya kocha Mikel Arteta, Arsenal walianza mchuano huo kwa matao ya juu huku Aubameyang na Nicolas Pepe wakimfanyiza kipa Vicente Guaita kazi ya ziada.

Ingawa hivyo, Palace walirejeshwa mchezoni na Christian Benteke aliyesawazisha katika dakika ya 50 baada ya ushirikiano wake na Jordan Ayew kumwacha hoi kiungo mkabaji Thomas Partey.

Palace walipachika wavuni bao la pili katika dakika ya 73 baada ya Conor Gallagher kumpokonya Albert Sambi Lokonga mpira kirahisi na kumwandalia Odsonne Edouard pasi safi.

Nusura Kieran Tierney asawazishie Arsenal katika dakika ya 80 ila akapaisha mpira licha ya kusalia peke yake na kipa wa Palace.

“Ilikuwa vigumu kuamini. Nilisikitika sana kuhusu jinsi masogora wangu walivyolegea katika sekunde za mwisho na kuwapa Arsenal fursa ya kusawazisha,” akasema Vieira.

Matokeo hayo yaliwapaisha Arsenal hadi nafasi ya 12 kwenye msimamo wa jedwali baada ya kutandaza mechi ya sita mfululizo ligini bila kushindwa. Kwa sasa wanajivunia alama 11, tatu zaidi kuliko Palace wanakamata nafasi ya 14.

Sawa na Palace, Arsenal pia walishuka ugani wakipania kujinyanyua baada ya kuokota alama moja pekee katika mechi ya awali. Arsenal walikuwa wameambulia sare tasa dhidi ya Brighton uwanjani Amex huku Palace wakikabwa koo na Leicester City kwa sare ya 2-2 ugani Selhurst Park kabla ya kipute cha EPL kusitishwa kupisha michuano iliyopita ya kimataifa kwa mujibu wa kalenda ya FIFA.

Japo Arsenal walilemewa na Palace katika kipindi cha pili, alama 11 kutokana na mechi tano zilizopita ni ishara ya kuimarika pakubwa kwa miamba hao wa zamani wa soka ya Uingereza walioanza kampeni za muhula huu kwa kusuasua.

Ushindi uliosajiliwa na Arsenal katika mechi tatu mfululizo za EPL dhidi ya Norwich City (1-0), Burnley (1-0) na Tottenham Hotspur (3-1) mwezi uliopita ni matokeo yaliyomvunia Arteta, 39, taji la Kocha Bora wa EPL mwezi Septemba.

Ufanisi huo uliwezesha mabingwa hao mara 13 wa EPL kujiondoa katika orodha ya vikosi vitatu vya mwisho jedwalini baada ya mwanzo mbaya uliowashuhudia wakipoteza mechi tatu za ufunguzi wa msimu dhidi ya Brentford (2-0), Chelsea (2-0) na Manchester City (5-0) kwa usanjari huo.

Arteta aliyechezea Arsenal mara 150 katika kipindi cha miaka mitano (2011-2016), aliteuliwa kuwa mrithi wa kocha Unai Emery mnamo Disemba 2019 na akaongoza klabu hiyo kutwaa Kombe la FA miezi mitano baadaye.

Kufikia sasa, ni pengo la alama tatu ndilo linatamalaki kati ya Arsenal na Palace ambao chini ya Vieira, wameshinda mechi moja, kuambulia sare mara tano na kupoteza michuano miwili kati ya minane iliyopita.

Vieira, 45, aliondoka Arsenal na kuyoyomea Italia kuvalia jezi za Juventus mnamo 2005, mwaka mmoja kabla ya kikosi hicho kutoka uwanjani Highbury na kuhamia Emirates. Nyota huyo wa zamani wa Ufaransa alikuwa nahodha wa kikosi cha Arsenal kilichonyakua ufalme wa EPL bila kushindwa katika mechi yoyote mnamo 2003-04.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

TAHARIRI: Mauaji ya kiholela ya wazee yakomeshwe

Ujanja wa kahaba wazimwa na mganga

T L