• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 4:54 PM
Kibicho aonya wahuni wanaopanga kusambaratisha sherehe za Mashujaa Kirinyaga

Kibicho aonya wahuni wanaopanga kusambaratisha sherehe za Mashujaa Kirinyaga

Na SAMMY WAWERU

SERIKALI imetoa onyo kali kwa wahuni wanaopanga kuzua fujo wakati wa maadhimisho ya Sikukuu ya Mashujaa 2021, yatakayoandaliwa kesho Kaunti ya Kirinyaga.

Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Karanja Kibicho ametahadharisha kwamba wenye mipango ya aina hiyo watakabiliwa kisheria.

“Tumepata habari kuna watu wanaopanga kuleta fujo, tunawaambia kuwa watu wa Kirinyaga hawatakubali na serikali haitakubali,” Dkt Kibicho akaonya.

Akitaja fujo hizo kama zinazolenga kuchochewa kisiasa, Katibu alisema serikali imepata taarifa za kijasusi wahuni hao watatolewa nje ya Kaunti ya Kirinyaga.

Rais Uhuru Kenyatta ataongoza taifa kuadhimisha sherehe hizo zitakazofanyika, katika Uwanja wa Wanguru, Kirinyaga.

Tayari kiongozi huyo wa nchi ametua katika kaunti hiyo, ambapo anaendelea kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo.

Naibu wa Rais Dkt William Ruto na kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga ambaye anaendeleza kampeni zake Meru kuwania urais 2022, pia watahudhuria.

Kufuatia athari za ugonjwa wa Covid-19, serikali imepiga marufuku hafla za maadhimisho hayo kuandaliwa katika kaunti zingine, kinyume na miaka ya awali ambapo kila kaunti imekuwa ikiandaa.

Kulingana na Dkt Kibicho, maandalizi ya hafla hiyo yamekamilika.

Awali, Mashujaa Dei ilitambulika kama Kenyatta Dei, ila ikabadilishwa chini ya Katiba ya sasa, iliyoidhinishwa 2010.

You can share this post!

Kanu yaimarisha kampeni mashinani

TAHARIRI: Mauaji ya kiholela ya wazee yakomeshwe

T L