• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
TAHARIRI: Serikali isidunishe uvaaji sare shuleni

TAHARIRI: Serikali isidunishe uvaaji sare shuleni

KITENGO CHA UHARIRI

JUHUDI za serikali kuhakikisha kila mtoto anapata elimu ya msingi na upili zinafaa kupongezwa.

Serikali imedhihirisha kwa vitendo kwamba inathamini elimu.

Waziri wa Elimu George Magoha amekuwa mstari wa mbele kuwasaka watoto ambao kufikia leo hawajaenda shuleni, karibu mwezi mzima tangu wenzao wajiunge na Kidato cha Kwanza.

Prof Magoha alipigwa na butwaa katika Kaunti ya Mombasa, alipowaona vijana wawili waliopata kati ya alama 350 na 395 wakiwa wangali nyumbani.

Picha zilimuonyesha waziri akiwa kwenye nyumba ya matope ya chumba kimoja, ambamo msichana aliyepata alama 355 alikuwa hajaenda shuleni kwa sababu ya matatizo ya kifedha nyumbani kwao.

Tukio hilo lilimthibitishia waziri yale ambayo Taifa Leo tumekuwa tukiyaangazia kuwahusu wanasiasa.

Viongozi wengi wamekuwa wakitumia basari na pesa nyingine za hazina wanazosimamia, kuwatuza wapambe wao wa kisiasa, watu waliowafanyia kampeni, marafiki, washirika katika biashara na matajiri walio na uwezo wa kulipa hata karo ya mwaka mzima.

Kama si hivyo, basi ilikuwaje mtoto aliyepata alama 394 au huyo wa 355 hakufanikiwa kupata basari katika eneobunge lake?

Mbali na basari ya mbunge, kuna basari ya kaunti. Hizo zote pamoja na wabunge wawakilishi wa kike hazikupatikana.Wasimamizi wa basari wanadai kwamba ili mtoto kupata ufadhili, ni sharti awe alisoma katika shule ya msingi ya umma.

Fikra hizo ni za kutaka kuonyesha kuwa wazazi wa mtoto aliyesoma shule ya kibinafsi wana uwezo. Si kweli. Hali ya maisha hubadilika. Covid-19 iliathiri biashara na shughuli mbalimbali.

Ingawa serikali inafanya kazi nzuri ya kuhakikisha watoto wote wamefika shuleni, yapaswa kutenga pesa za kuwanunulia sare wale walio na hali ngumu kabisa. Kuwaamuru walimu wakuu wawapokee wanafunzi wote hata kama hawana sare, si suala la busara.

Shule ni pahali ambapo watoto wote hutakiwa wawe sawa kupitia sare.

Kufanya hivyo hufanya iwe rahisi kwa walimu kuwatambua wanafunzi wao, hata kunapokuwa na mkusanyiko wa shule mbalimbali.

Kuvaa sare pia huepusha wahuni na watu wasiokuwa wanafunzi kuingia shuleni.

Kwa hivyo serikali itafute mbinu nyingine za kuwasaidia watoto maskini, lakini si kusoma bila ya sare.

You can share this post!

Maandalizi ya KCB Machakos Rally yapamba moto

Tarus, Bitok wataja vikosi vya Kenya vya voliboli kuwania...