NA RICHARD MAOSI
MCHEZO wa Sataranji almaarufu Chess unaweza kuchezwa na kundi la watu wenye umri wowote, sehemu yoyote ikiwemo ndani na nje ya mitandao.
“Huu ni mchezo ambao unaweza kuwafaa wanafunzi ambao wanalenga kuongeza makali katika somo la Hisababti na Sayansi, ikizingatiwa kuwa humhitaji anayecheza kufikiri sana,” anasema Colleen Wanjiku mwanafunzi mwenye umri wa miaka 11 katika shule ya msingi ya Roots Academy, Nakuru.
Wanjiku anasema alianza kujifunza chess akiwa na umri wa miaka minane, baada ya babake kumtambulisha kwenye mchezo huo.
Alipojiunga na shule ya msingi ya Roots aliupa mchezo wa chess kipaumbele, ingawa kulikuwa na michezo mingineyo kama vile soka, hoki na uogeleaji.
Mapenzi haya ya dhati kwa chess yalimsukuma kuweka juhudi zake zote akiamini kuwa siku moja atakuja kuwa mchezaji bora wa kiwango cha kimataifa.
Hata hivyo, anasema chess nje ya mtandao wa kijamii ndio njia bora zaidi ya kujinoa ikizingatiwa kuwa mchezaji atakuwa katika nafasi nzuri ya kujitambua katika kiwango cha kibinafsi.
Aidha, husaidia kukidhi mahitaji ya viwango vyote vya mchezo kwa kupata uzoefu kamili na kujirudi katika kila hatua.
Kwa mujibu wa Wanjiku, yeye hufanya mazoezi kila siku wakati wa jioni, siku za wikendi na wakati wa siku za vyama shuleni.
Mwalimu wake Bw Rodrick Marando anasema bidii za mwanafunzi wake zimempa fursa nyingi za kutambulika kwenye kaunti ya Nakuru, mara hii akijiandaa kushiriki kwenye mashindano ya Nakuru Chess Club yatakayofanyika Machi mwaka huu.
Aliongeza kuwa desturi ya kucheza chess huwa ni nyepesi kwani kila mchezaji huwa anapaswa kudhibiti jeshi la ala 16, ambapo mchezaji mmoja huwa na ala nyeupe huku mwingine akiwa na ala nyeusi.
Pili, Wanjiku anashauri kuwa hatua ya kwanza alipojifunza kucheza chess alizingatia namna ya kushika bodi na jinsi ya kusogeza ala hizi kwenye bodi, hii ikiwa ni katika hatua muhimu ya kuanzisha mchezo vyema.
Tangu anze kushiriki mchezo wa chess, umemsaidia kutuliza mawazo yake ikiwa ni baada ya muda mrefu wa kushinda darasani wiki nzima akidurusu.
Aidha, amekuza weledi wake wa lugha na kuimarika katika somo la Kiingereza na Kiswahili , hii ikitokana na umahiri wake wa kujieleza.
Desturi ya mchezo wa sataranji humfanya mshiriki afikiri sana. Hata hivyo, ili aweze kubobea na kutopea anatakiwa kushiriki kwenye michuano mingi ya kirafiki ndani na nje ya shule yake.
Subscribe our newsletter to stay updated