• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
Udaku: Neymar aponda raha na vipusa kilabuni huku mkewe mjamzito akihangaika

Udaku: Neymar aponda raha na vipusa kilabuni huku mkewe mjamzito akihangaika

VITUKO VYA MASTAA WA MAJUU NA CHRIS ADUNGO

MREMBO Bruna Biancardi, 29, amekiri “kufadhaishwa sana” baada ya kusambaa kwa video zilizoonyesha dume lake Neymar, 31, likiponda raha na vipusa wawili katika kilabu usiku.

Fowadi huyo mzoefu raia wa Brazil amekuwa akitoka kimapenzi na mwanamitindo Bruna tangu 2021, japo waliweka parwanja uhusiano wao Januari mwaka jana.

Kwa sasa Bruna ana ujauzito wa miezi minane na miamba hiyo ni ya mtoto wake wa kwanza pamoja na Neymar, aliyebanduka Paris Saint Germain (PSG) muhula huu kuyoyomea Al-Hilal ya Saudi Arabia.

Video zilizomkoroga nyongo Bruna ni za Neymar akipapasana na visura wawili wasiofahamika, ambao walikuwa wakimpiga pambaja na mabusu motomoto katika karamu iliyoandaliwa mkahawa mmoja wa kifahari nchini Uhispania, wiki jana.

Tukio hilo lilimchochea Bruna kuingia Instagram: “Habari za mchana? Ninajua kilichotokea na nimesikitishwa sana. Lakini katika hatua ya mwisho ya ujauzito wangu mawazo yangu ni kwa mtoto huyu wa kike anayekaribia kutua duniani!”

Staa wa zamani EPL jela kwa kumtupia mchumba makonde

ALIYEKUWA mwanasoka wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Ognjen Koroman, ametiwa nguvuni kwa tuhuma za kumpiga na kumjeruhi mchumba wake wa zamani.

Mserbia huyo aliwahi kuunogesha EPL mnamo 2006 akichezea Portsmouth mara sita, kabla kuhamia Red Star Belgrade ya Serbia.
Kwa mujibu wa gazeti la Sportal nchini Serbia, Koroman, 45, alizuiliwa na maafisa wa polisi asubuhi ya Alhamisi wiki jana.

Anadaiwa kumshambulia kidosho Ana Micic, kumtemea cheche za maneno na kumuachia majeraha makali ya kimwili baada ya kumtandika mateke na makonde ubavuni.

Jude Bellingham: Wa kushoto au kulia, itakuwaje?

KIUNGO mvamizi wa Real Madrid na timu ya taifa ya Uingereza, Jude Bellingham, 20, ametemana tena na kidosho raia wa Amerika, Azra Mian.

Bellingham alianza kumtambalia Azra, 22, mwishoni mwa muhula uliopita baada ya kukutana kwenye programu ya Raya, ambayo ni maarufu miongoni mwa wanaotafuta wachumba mitandaoni.

Nyota huyo — aliyejiunga na Real Madrid majuzi baada ya kuagana na Borussia Dortmund — alianza kutoka na Azra baada ya kutengana na mwanamitindo Asantewa Chitty, aliye na usuli wa Uturuki na Ghana.

Hata hivyo, tetesi zilidai wiki jana kwamba Bellingham amemrudia Chitty baada ya kumtoka Azra.
Awali kiungo huyo Muingereza alipakia mitandaoni picha alizowahi kupigwa pamoja na Chitty, 24, na kuambatisha mchoro wa pete.

Chini ya picha aliandika: “Barafu ya moyo wangu na mama mtarajiwa wa watoto wangu ni wewe A.C. Huu ni mwaka wa ndoa kati yetu. Ilikuwa vyema kufahamiana na Azra!”

Naye Chitty akatumia Instagram kufichua ukubwa wa penzi lao.

“Nakustahi kwa pendo halisi. Sitaki iwe siri. Nashindwa kujizuia. Natazamia siku hiyo kwa hamu,” alihoji.
Kwa mujibu wa mdokezi kutoka familia ya Bellingham, Chitty alikuwa mgeni wa mara kwa mara jijini Madrid na sasa wanapanga kutambulishana kwa wazazi.

  • Tags

You can share this post!

Hizi mbinu zimesaidia wengi kukabili hali ngumu ya uchumi

Kampuni za Tetra Pak na PAKPRO zashirikiana kugeuza kero ya...

T L