NA SAMMY WAWERU
WASHIRIKA katika sekta ya ufugaji wameirai serikali kuondoa kwa muda ushuru na ada zinazotozwa malighafi ya chakula cha mifugo.
Kenya huagiza kutoka nje malighafi inayotumika kutengeneza malisho ya mifugo, na tangu janga la Covid-19 litue uhaba wa bidhaa hizo unashuhudiwa.
Zinajumuisha, mahindi, soya, ngano, shayiri, alizeti, mbegu za pamba, miongoni mwa nyingine.
Kenchic, kampuni tajika hapa nchini na Ukanda wa Afrika Mashariki katika ‘uzalishaji’ wa kuku, inasema biashara ya ufugaji imegeuka kuwa ngumu kufuatia mfumko wa bei ya chakula.
“Tunapitia kipindi kigumu, ikizingatiwa kuwa huagiza malighafi nje ya nchi. Ni haba, na yanayopatikana ni ghali,” amesema Bw Jim Tozer, Mkurugenzi Mkuu.
Chini ya kipindi cha muda wa miaka miwili, viwanda visivyopungua 40 vya kusaga na kuunda chakula cha mifugo vimefungwa kutokana na hali ngumu na mazingira mabovu ya biashara.
Isitoshe, baadhi ya wafugaji hususan wa kuku wamelewa kuendeleza biashara, changamoto ambazo zimechangia ongezeko la bei ya kuku na mayai.
Mfano, kuku wa kienyeji aliyeboreshwa na aliyekuwa akiuzwa Sh500, amepanda sasa akichezea kati ya Sh600 – 700.
“Tunachoomba, serikali iondoe kwa muda ushuru na ada zinazotozwa malighafi ya chakula cha mifugo,” akahimiza Bw Martin Kinoti, Katibu Mkuu Muungano wa Viwanda vya Kutengeneza Malisho ya Mifugo Nchini (Akefema).
Wafugaji aidha pia wanaomba serikali kuzindua mpango wa ruzuku, kwa chakula cha mifugo.
Bw Tozer, anahakikishia wateja wa Kenchic kwamba kampuni hiyo haitaongeza bei ya bidhaa zake.