• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 11:30 AM
‘Usilaze damu mwanamke wewe’ 

‘Usilaze damu mwanamke wewe’ 

Na WINNIE A ONYANDO

“MUME wangu anahanya” ni kauli ambayo utasikia kutoka kwa vinywa vya wanawake wengi walio katika ndoa.

Rosey, 25, ni mwanadada mrembo ambaye pamoja na mumewe Paul, wamejaliwa mtoto mmoja wa kiume.

Kipusa huyo anamlaumu mumewe na kumchukia kwa tabia yake ya kuchepuka.

Ingawa si tabia nzuri kidini na kijamii, kuna sababu nyingi zinazoweza kumfanya mwanamume achepuke.

Unaweza ukawa wewe ni mwanamke mrembo kupindukia kama Rosey lakini unashindwa kwa nini mume wako anakuendea kinyume.

Wakati vitendo vya kuchepuka ni vya kulaaniwa, ukweli ni kuwa baadhi ya wanawake hawawajibiki jinsi ipasavyo wakiwa katika ndoa.

Mwanamke hafai kuwa yeye ndiye sehemu ya tatizo huku anamlaumu mume eti ana jicho la nje.

Ukweli ni kwamba baadhi ya wanawake wenyewe wamekuwa chanzo cha waume kurambwa miguu na mbwa.

Wakati wa kuchumbiana, utamuona mwanadada ni malaika, hana shida wala dosari. Mwanamume anashawishika “bila shaka huyu ni mchumba mzuri” na kuanza kuharakisha pilkapilka za kufunga pingu za maisha na kipusa huyo.

Kitumbua kinaingia mchanga wakati mke wa huyo mwanamume anaamua kuwa ‘yeye’ ambapo anatoa rangi yake kamili. Kumbe alikuwa kinyonga sasa amebadilika!

“Simwelewi kabisa mume wangu Paul kwa sababu zamani akinijali na kunifurahisha kipindi tunachumbiana. Sasa amekuwa kigeugeu, simtambui kamwe,” Rosey analalamika.

Rosey anamshuku mumewe kuwa ana ‘mpango wa kando’ ila yeye mwanamke mwenyewe hajajichunguza kutathmini kinachoweza kusababisha mumewe kuwa katika uhusiano wa kimahaba na mwanamke mwingine.

Kuna vijisababu vingi vinavyoweza kuwafanya wanaume kuwa walaghai na kuanza kutoka kimapenzi na wanawake wengine mbali na wake.

Mwanamke pindi tu anapojifungua, analegeza kamba ya usafi na kushughulikia mwili na urembo wake. Anasema kuwa ‘tayari ashapatikana’ ila hajui kuwa wanaume ni viumbe wanaovutiwa na wanachoona au wanayemuona.

Kazi yake katika nyumba ni kumshughulikia mtoto na nyumba, utadhani aliolewa “kuridhisha tu kazi za nyumba” huku akimpuuza mume.

Usilaze damu mwanamke wewe. Mpe mumeo muda mwingi, ukae karibu naye na umdekeze jinsi inavyofaa.

Tengeneza mwili wako, jipambe ili urudishe usichana wako. Mume akirejea nyumbani jioni asije akakupata ukinuka jasho, hujakoga wala hujipamba.

Mpe sababu za kuwa na hamu ya kuja nyumbani.

Mtayarishie chakula katika mazingira safi, mpe chakula kwa njia ya utaratibu. Usimtupie chakula kana kwamba yeye ni mbwa. Hata mbwa wa matajiri hawatupiwi chakula! Ukarimu wako utamtoa ‘ulafi wa fisi’ na kumfanya kuwa na roho ya kutosheka, hata akiwaona warembo wengine nje hana haja.

Unapojitunza kama mwanamke, utampa mume wako hamu ya kutaka kuwa kando yako kila wakati. Hatakuwa na tamaa anapowaona wanawake wengine huko nje.

Mpumbaze na umfunike na blanketi ya mapenzi. Yaani atazama katika bahari ya mapenzi akiona raha ajabu!

Akirejea nyumbani asikutane na nguo zimetapakaa kila mahali, nyumba imechakaa, watoto ni wachafu ilhali wewe kazi yako ni umbea na kurandaranda tu.

Jishughulishe mwanamke ili uweze kuilinda ndoa yako.

You can share this post!

SHINA LA UHAI: Dhiki ya wagonjwa huku vikwazo vya Covid...

Omala ajiandaa kwenda Uswidi kusakatia Linkoping City