KWA HISANI YA KENYA YEAR BOOK
ILIIBUKA wazi kuwa kutokana na rambi rambi zake katika mazishi ya Moi mnamo Februari 2020, kwamba Sally Kosgei anajua mengi kuhusu sio tu kazi, ubishi na zilikofeli serikali za Kenya zilizopita lakini pia anafahamu ukweli wa hali ya siasa ambazo serikali hizo zilipitia.
Zaidi, anafahamu mengi kuhusu wana wa wanasiasa na wafanyabiashara wa Kenya, baadhi ambao kwa wakati huu wanaoshikilia nyadhifa za juu serikalini na wengi ambao aliwalea tangu enzi alizokuwa balozi wa Kenya nchini Uingereza miaka ya tisini.
Kosgei pia anafahamu mengi kuhusu siasa za Amerika akiwa alisoma na Waamerika wenye majina makubwa kama Condoleezza Rice, ambaye alikuwa Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Amerika katika Stanford, na kuwa rafiki wa chanda na pete wa Jendayi Frazier na raia wengine mashuhuri wa Amerika wasomi na walio katika katika utumishi wa mashauri ya Kigeni.
Hata hivyo, Wakenya watasubiri kwa muda mrefu kabla ya kupata anayojua kwa undani, kwa kuwa hajachapisha kitabu kuhusu maisha yake.
Kwa mbali, Kosgei anaonekana mtulivu lakini punde mtu anafahamu kuwa hii ni hulka ya balozi aliyebobea.
Ni mtu mwerevu anayefahamu mengi kuhusu masuala na matukio muhimu Kenya na kote ulimwenguni. Si ajabu anasifiwa kama mmoja wa viongozi wenye ushawishi na nguvu baada Kenya kupata uhuru.
Sifa hizi zilidhihirika mwaka wa 2008 alipochaguliwa kuwa mwanachama wa timu ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM) iliyotwikwa jukumu la kufanya mazungumzo na wenzao wa chama cha Party of National Unity (PNU) katika juhudi za kukomesha ghasia za baada ya uchaguzi zilizokumba maeneo ya Rift Valley, Nyanza na Nairobi baada ya uchaguzi mkuu wa 2007.
Kuchaguliwa na ODM kujiunga na timu hiyo muhimu kulionyesha kuwa ujuzi, uongozi, ukali na uthabiti wake ulihitajika katika mazungumzo kama hayo. Lakini pia inaweza kuwa alichaguliwa kwa sababu ya ufahamu wake mpana kuhusu serikali. Kutokana na mafunzo na tajiriba yake katika serikali na kibalozi, Koskei anatosha kuwa katika orodha ya watu mashuhuri barani Afrika.
Baada ya Muafaka wa Kitaifa kutiwa saini, Kibaki alimteua Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia (MoEST) katika serikali ya muungano iliyoundwa baada ya majadiliano ambayo alihudumu kwa miaka miwili kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Kilimo.
Dkt Sally Jepngetich Kosgei alizaliwa katika eneo bunge la Aldai katika Wilaya ya Nandi katika familia ya wakulima.
Katika mahojiano na Kitabu kuhusu Bunge la Kumi, Kosgei alisema kwamba wazazi wake walimhimiza kuongoza kila kitu alichohusika nacho na hivyo basi kuweka msingi wa maisha yake ya uongozi.
Katika rambi rambi zake alifichua kwamba ufanisi wake katika elimu ulitokana na Moi anayesema alimfanya aahidi kuendelea na masomo yake hadi kiwango cha uzamifu.
Alisomea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Tanzania, kabla ya kuelekea Stanford alikosomea digrii ya Uzamili na Uzamifu katika Diplomasia na Masomo ya Afrika. Baada ya kurejea Kenya alifanya kazi kama mtumishi wa cheo cha chini katika umma kabla ya Moi kumfungulia kazi yake ya diplomasia kwa kumteua kusimamia balozi za Kenya kati nchi tofauti kabla ya kumteua Waziri wa Mashauri ya Kigeni.
Moi alimteua Mkuu wa Utumishi wa Umma miaka yake ya mwisho uongozini kabla ya kustaafu 2002. Wadhifa wa Mkuu wa Utumishi wa Umma ulikuwa wenye nguvu zaidi wakati huo kuliko hata wa Makamu Rais. Kwamba hakutumia wadhifa huo kuweka vizingiti kwa mpito hadi utawala mpya wa Mwai Kibaki ni kuonyesha uzalendo wake.
Aligombea kiti cha kisiasa kwa mara ya kwanza 2007 na kuchaguliwa mbunge wa eneo bunge la Aldai alilowakilisha kati ya 2008 na 2013.
Subscribe our newsletter to stay updated