NA CHARLES WASONGA
KUFUATIA visa vya wazee kuuawa baada ya kupokea pesa za mpango wa Inua Jamii, ipo haja kwa serikali kuchukulia kwa uzito zaidi suala la usalama wa wakongwe.
Wazee hao wenye wa miaka 70 na zaidi sasa wanaishi katika kiwewe kwa kulengwa na wakora sababu ya pesa hizo.Juzi, wazee waliosajiliwa kwa mpango huo kote nchini walipokea Sh8,000 kila mmoja.
Haya ni malimbikizo ya malipo ya miezi minne kwani hupokea Sh2,000 kila mwezi.
Mara ya mwisho wakongwe hao, ambao pia hujumuisha walemavu na mayatima, kupata kiinua mgongo hicho ilikuwa Juni 2022.
Idara inayohusika na maslahi ya wakongwe katika Wizara ya Leba ilisema malipo ya Novemba na Desemba yatakuja baadaye.
Huku kucheleweshwa kwa pesa hizo ndiko kunaweka wazee katika hatari ya kushambuliwa na wakora, kuporwa pesa zao na hata kuuawa kinyama ilivyoripotiwa wiki hii.
Kwa sababu habari za kutolewa kwa pesa hizo hutangazwa katika vyombo vya habari, wahalifu hujua siku mahususi ambayo watalipwa na kiasi cha pesa watapokea.
Kwa msingi huo, serikali ya kitaifa kupitia maafisa wa utawala nyanjani – kuanzia machifu na manaibu wao – wanafaa kuwalinda wazee, hasa wanaoishi pekee yao.
Manaibu wa chifu wanaweza kushirikiana na wazee wa vijiji na wanachama wa mpango wa Nyumba 10 kutimiza hilo.
Hili linawezekana ikizingatiwa kuwa idadi ya wakongwe wanaoishi peke yao kijijini sio kubwa zaidi, hivyo wanajulikana.
Ikiwa maafisa hao wa utawala wangelikuwa wamechukua hatua kama hii kuwalinda wazee, kuna uwezekano mkubwa Cheruiyot Cherono wa Kitumbei kutoka Baringo ya Kati, Kaunti ya Baringo, hangeuawa.
Naamini kuwa kando na visa vichache vya kushambuliwa kwa wazee, ambavyo vimeripotiwa katika gazeti hili na vyombo vingine vya habari, kuna visa vingine sawa na hivyo ambavyo vimetokea lakini havijanakiliwa na wanahabari.
Subscribe our newsletter to stay updated