NA CHARLES WASONGA
BAADHI ya mawaziri wapya walioingia afisini juzi wanawakanganya maafisa wa umma katika wizara zao na Wakenya kwa ujumla, kutokana na kauli nzito wanazotoa kiholela katika mikutano ya hadhara.
Kimsingi, mawaziri hawa wanatoa kauli na maagizo ya kisera ambayo yanapaswa kwanza kujadiliwa katika baraza la mawaziri, chini ya uenyekiti wa Rais William Ruto kabla ya kutolewa rasmi kwa umma.
Mawaziri ambao ninawarejelea hapa ni; Waziri wa Biashara Moses Kuria, Aisha Jumwa (Utumishi wa Umma na Masuala ya Jinsia) na Ezekiel Machogu (Elimu).
Mnamo Jumanne wiki jana, Bw Kuria alitangaza kuwa serikali ya Kenya Kwanza itapiga marufuku uagizaji na uuzaji wa nguo kuukuu, almaarufu mitumba, baada ya kufufua sekta ya utengenezaji nguo.
Akiongea wakati wa tamasha ya kuvumisha nguo zinazotengenezwa humu nchini, Changamka Shopping Festival, katika jumba la KICC, Nairobi, Waziri Kuria, hakuelezea ni lini marufuku hayo yataanza kutekelezwa au wakati ambapo serikali itafaulu kufufua viwanda vya kutengeneza nguo.
Hii ndio maana mbunge wa Kamukunji, Bw Yusuf Hassan, anayewakilisha wafanyabiashara wa mitumba wanaohudumu katika Soko Kuu la Gikomba, aliiponda serikali ya Rais Ruto kwa kile alidai ni kwenda kinyume na ahadi yake ya kupiga jeki biashara ya mitumba inayotegemewa na Wakenya wengi wa tabaka la chini.
Itakumbukwa kwamba suala kuhusu hatima ya biashara ya mitumba lilikuwa kiazi moto wakati wa kampeni kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022 baada ya aliyekuwa mgombea urais wa Azimio la Umoja-One Kenya Raila Odinga, kudai nguo za mitumba ambazo huletwa nchini ni zile ambazo zilivaliwa na wafu katika mataifa ya Uropa na Amerika.
Dkt Ruto, wakati huo akiwa Naibu Rais na mgombea urais wa muungano wa Kenya Kwanza, aliongoza vigogo wenzake, akiwemo, Bw Kuria, kumshambulia Bw Odinga kwa kuwadunisha mahasla ambao hutegemea biashara ya mitumba.
Kwa hivyo, Waziri Kuria angechelea kuzungumzia suala hilo, kabla ya kujadiliwa na kupitishwa katika baraza la mawaziri.
Siku hiyo hiyo ambayo Bw Kuria alikuwa akitoa kauli kuhusu mitumba, mwenzake, Bi Jumwa aliamuru kwamba vituo vyote 52 vya Huduma Centre kuhudumu kuanzia saa moja asubuhi hadi saa moja za usiku.
Hii ni licha ya kwamba Sheria ya Leba ya 2007 inasema wazi kwamba watumishi wa umma wanapaswa kufanya kazi kwa muda wa saa nane.
Kando na hayo, Bi Jumwa aliahidi kuhakikisha kuwa Mishahara ya Watumishi wa Umma wanaongezwa mishahara, baada ya muda wa siku 100.
Inasikitisha kuwa kwa kutoa kauli hiyo, Waziri huyo alionekana kutofahamu kulingana na Katiba, ambayo aliapa kuilinda na kuitetea, wajibu wa kuongeza mishahara ya watumishi wa umma ni wa Tume ya Kukadiria Mishahara na Marupurupu (SRC) wala sio wake kama Waziri.
Waziri Machogu naye ametangaza kuwa serikali ya kitaifa itasitisha ufadhili kwa vyuo vikuu vya umma, ilhali suala hili la kisera halijajadiliwa na kupitishwa katika baraza la mawaziri.
Kauli hii ambayo aliitoa wiki jana katika ziara yake kaunti ya Nyeri ni lenye uzito mkubwa kwani kimsingi, linageuza vyuo vyote 73 vya umma na mabewa yao, kuwa vyuo vya kibinafsi.
Nawaomba mawaziri hawa wapya wapunguze msisimko unaotokana na teuzi zao na wakome kutoa kauli au amri za kiholela zinazokinzana na mamlaka yao.
Subscribe our newsletter to stay updated