NA KINYUA KING’ORI
HATUA ya Rais William Ruto kukubali baadhi ya hoja zilizochochea maandamano ya muungano wa upinzani Azimio, ni nzuri.
Hoja hizo zinafaa kusikizwa na kujadiliwa bila kujali nani aliyesahihi au aliyekosea kuhusu suala la kutisha maandamano nchini.
Katika muktadha huo napongeza Azimio, ikiongozwa na Bw Raila Odinga, kwa kusitisha masi hayo ili kutoa nafasi ya majadiliano.
Kwa kutathmini hasara, uharibifu na uvamizi ulioshuhudiwa wakati wa maandamano, kamati itakayoundwa kutafuta suluhu haifai kuwa na misimamo mikali. Iwe kamati ya wanachama wenye moyo wa hariri ili watambue upesi masuala tata na jinsi ya kuyatatua, sio tu kuzuia maandamano bali pia kuokoa raia wanaoteseka sababu ya ugumu wa maisha.
Wananchi hawatarajii juhudi hizo za maridhiano kukumbwa na vizingiti maana wamechoshwa na maasi na igawanyiko nchini.
Inafurahisha kuona Dkt Ruto ametambua ni wajibu wake kuhakikisha yuko mstari wa mbele kuleta amani na utulivu kwa kushirikisha viongozi wa upinzani kufaulisha taifa. Kweli maandamano ni haki ya kikatiba ila inatia hofu yanapojaa vurugu kiasi cha kuingilia uhuru wa wengine wanaondelea na shughuli zao muhimu hasa wafanyabiashara.
Katika taifa linaloheshimu demokrasia, viongozi serikalini na upinzani huwa na mtindo wa kujadiliana kwa manufaa ya kuboresha maisha bila kuzingatia mirengo ya kisiasa. Hivyo mazungumzo hayo ni mazuri ila tu yalenge kuwafaa raia na kuimarisha utendakazi wa asasi huru nchini kama vile Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Ni wajibu wa viongozi kudumisha umoja na amani kwa kushirikiana kwa upendo bila unafiki.
Wote watakaoshirikishwa katika mazungumzo hayo wajue raia wanataka amani, gharama ya maisha ishuke , maridhiano na mazingira bora ya kuendelea na shughuli zao bila usumbufu wa maandamano yasiyoisha yanayohatarisha udhabiti wa uchumi na usalama wa taifa.
Hatua hiyo itakuwa imeleta suluhu kuzuia hali ambayo viongozi wa upinzani hujiona kama juhudi na michango yao kwa taifa haitambuliwi na serikali kiasi cha kujitolea kufanya lolote yakiwemo maandamano, kuikashifu na kuiharibia sifa ili ionekane kama iliyofeli kutekeleza ahadi zao na kutojali raia.