• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
NGILA: Tumia ufadhili wa Google kupiga jeki biashara yako

NGILA: Tumia ufadhili wa Google kupiga jeki biashara yako

Na FAUSTINE NGILA

IWAPO wewe ni mjasiriamali katika sekta yoyote na unatumia teknolojia, basi huna budi kutabasamu kwa kuwa kampuni ya teknolojia ya Google imejiandaa kukupiga jeki.

Kwa kutambua umuhimu wa biashara za wastani na zile ndogondogo katika ukuaji wa uchumi, kampuni hiyo imetenga Sh1 bilioni kuinua biashara hizo ambazo zilipata pigo kuu kutokana na janga la corona.

Hii ni ithibati kuwa ukitia bidii katika ubunifu wako wa kila siku, kuna manufaa fiche ambayo utakumbana nayo katika safari yako ya ujasiriamali.

Tofauti na mikopo ya benki za humu nchini ambayo hutoza riba ya juu, fedha za Google zitapeanwa kwa riba ya chini, ikizingatiwa biashara nyingi zimekuwa zikipata hasara kutokana na kuporomoka kwa uchumi.

Ni bayana kuwa wafanyabiashara wengi wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii na majukwaa ya kidijitali kunadi bidhaa na huduma zao, lakini wengi wamefunga biashara hizo kutokana na ukosefu wa hela za kulipia kodi na umeme.

Mataifa mengine yaliyochaguliwa Afrika ni Afrika Kusini, Ghana na Nigeria, ishara kuwa wafadhili wako tayari kuwasaidia wananchi wanaojituma kila siku katika ubunifu wa teknolojia za kuziba changamoto zilizoko katika jamii.

Kwa wale ambao kazi yao ni kulalamika kuwa hakuna ajira, sasa waanze kufikiria kuhusu kuunda suluhu za kibiashara ambazo zinaweza kuchangia katika kubuni nafasi za kazi.

Nasema hivi kwa kuwa nimetangamana na vijana wengi waliohitimu elimu ya chuo kikuu lakini uzembe wa kufikiria umewatuma kusaka ajira katika kampuni huku wengine wakisalia mitaani kulia kuwa ufisadi serikalini ndio chanzo cha wao kukosa ajira.

Nawasikitikia sana vijana wanaofikiria hivi, kwa vile wana akili shupavu na elimu ya kutosha kuwawezesha kufikiria kuhusu miradi ya ubunifu ya kukabiliana na matatizo yaliyoko katika sekta za afya, elimu, uchukuzi, mawasiliano, fedha, kilimo, mazingira, sheria na hata uvuvi.

Kwa miaka minne, wahadhiri wao hawakuwaambia kuwa lengo kuu la kwenda chuoni ni kuunda nafasi za kazi na wala si kusaka ajira, na sasa bado wanaamini kuwa ipo siku wataajiriwa.

Kulingana na jinsi kasi ya teknolojia inavyotafuna nafasi za ajira viwandani, vijana wanafaa kufikiria kuwa katika mstari wa mbele katika uundaji wa teknolojia hizo, la sivyo watasalia kulia kuwa maisha ni magumu.

Utalemewaje kusajili biashara yako ndogo wakati wafadhili wa humu nchini na kigeni wamejaa kila kona wakisubiri kuona mapendekezo yako ya bishara ili wakupe mamilioni ya ufadhili?

Umaskini miongoni mwa vijana ni wa kujitafutia kwa kuwa wako na nguvu inayohitajika, lugha ya kuandika na kuelezea mapendekezo na akili ya kusimamia biashara hadi iimarike. Lakini wengi hawataonja hata shilingi moja ya Sh1 bilioni zilizotolewa na Google.

Usiniambie eti umetoka familia maskini na uko na digrii yako pale nyumbani na huna ajira.

Gutuka usingizini, ingia kwenye intaneti, saka changamoto zinazolemea serikali na jamii, fikiria kuhusu miradi ya kumaliza matatizo hayo.

Utanishukuru baadaye kwani utafiti wako utakuelekeza kwa mchakato wa kutengeneza pendekezo ambalo utatumiwa mamilioni kwenye akaunti yako ya benki ili uunde ajira kwa wenzako waliotekwa na laana ya kutofikiria. Kazi kwako.

You can share this post!

Obado na watoto wake wanne kujibu mashtaka ya ufisadi wa...

WASONGA: Sherehe bila kusaidia familia za mashujaa ni kazi...

T L