• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 1:46 PM
TAHARIRI: Magavana wapya wakague madeni ya zamani ili wasilipie huduma, bidhaa hewa

TAHARIRI: Magavana wapya wakague madeni ya zamani ili wasilipie huduma, bidhaa hewa

NA MHARIRI

JANA Alhamisi magavana 45 waliapishwa baada ya kuibuka washindi katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.

Baadhi ya magavana walioapishwa watakumbana na rundo la madeni, bajeti kubwa ya mishahara, miradi iliyokwama na migomo ya mara kwa mara ya wafanyakazi miongoni mwa changamoto nyinginezo.

Magavana Susan Kihika (Nakuru), Johnson Sakaja (Nairobi), James Orengo (Siaya), Jonathan Bii (Uasin Gishu), Jeremiah Lomurkai (Turkana), Kiarie Badilisha (Nyandarua), Jonathan Leleliit (Samburu), Hassan Guyo (Isiolo) na Irungu Kang’ata (Murang’a) ni baadhi tu ya wale watakaokabiliwa na changamoto tele wanapoingia ofisini kujenga kaunti zao.

Magavana hawa wanaoanza kuhudumu muhula wa kwanza wanakabiliwa na madeni ya kima cha Sh130 bilioni yaliyoachwa na watangulizi wao.

Kulingana na wataalamu wa masuala ya uongozi, mizigo ya madeni ambayo magavana hao wapya wamerithi itaathiri uwezo wao wa kutekeleza miradi ya maendeleo waliyoorodhesha katika manifesto zao.

“Hii ni kwa sababu, kwa mujibu wa Sheria za Usimamizi wa Fedha za Umma, 2012, itawalazimu kulipa madeni hayo, japo uhalali wa madeni mengine ni wa kutiliwa shaka,” anasema Bw Barasa Nyukuri.

Kaunti ya Nairobi ni miongoni mwa zile ambazo zinazongwa na mzigo mkubwa wa madeni.

Kulingana na ripoti kuhusu Utekelezaji wa Bajeti katika Serikali za Kaunti (CGBR), kaunti ilikuwa na madeni ya kima cha Sh84.94 bilioni kufikia Juni 30, 2022.

Kaunti zingine zenye madeni makubwa ni kama vile, Kiambu (Sh5.21 bilioni), Mombasa (Sh 4.82 bilioni), Wajir (Sh 3.82 bilioni), Machakos (Sh2.80 bilioni) na Tana River (Sh2.41 bilioni).

Magavana wapya pia watakumbana na bajeti kubwa ya mishahara ya wafanyakazi, hali ambayo itaathiri uwezo wao wa kutekeleza miradi ya maendeleo.

Kwa mfano, katika mwaka wa kifedha wa 2021/2022, kaunti nyingi zilielekeza kiasi kikubwa cha pesa katika matumizi yasiyofungamana na maendeleo kama vile ulipaji mishahara ya wafanyakazi.

Kulingana na ripoti iliyotolewa na Msimamizi wa Bajeti, Dkt Margaret Nyakang’o Juni 2022, kaunti zilizotumia pesa nyingi kwa matumizi yasifungamana na miradi ni; Nakuru, Samburu, Baringo, Narok, Kericho, Trans Nzoia, Uasin Gishu, West Pokot Magharibi, Elgeyo Marakwet na Laikipia.

Jana Alhamisi, gavana Irungu Kang’ata aliapa kutolipa madeni hadi yakaguliwe.

Magavana wengine wanapaswa kumwiga Kang’ata ili kuhakikisha kuwa hawalipi madeni hewa.

  • Tags

You can share this post!

Magavana wapya wachukua usukani na kuahidi mengi

Njaa kuzidi kuathiri Pembe ya Afrika

T L