NA MHARIRI
KUGUNDULIWA na kufukuliwa kwa makaburi ya halaiki ya watu wanaoshukiwa kuwa wafuasi wa mhubiri Paul Makenzie huko kaunti ya Kilifi kunaonyesha kupanuka kwa mafunzo yenye itikadi kali na athari zake hasi kwa jamii.
Kufikia jana Jumapili, idadi ya miili ya wafu wanaoaminika waliangamia wakiwa kwa mfungo wa kutokula wala kunywa iliyofukuliwa katika makaburi ilifika 39.
Hii ni baada ya miili 18 kufukuliwa, huku idadi ikiendelea kuongezeka. Uvumbuzi huu unatia kwenye mizani imani za kidini na kuibua haja ya kuchukuliwa kwa hatua za kuzuia maafa zaidi siku zijazo. Kusababisha watu kujitesa kwa njaa hadi kufa kwenye msitu huku wakishikilia imani kwamba kufanya hivyo ni kutekeleza mapenzi ya Mungu ni ukatili wa hali ya juu ambao haupaswi kuruhusiwa. Japo ni vigumu kuzuia mtu kufuatia imani ya kidini katika nchi inayotoa uhuru wa kuabudu, kuna haja ya kuhakikisha utimamu wa akili za viongozi wa kidini na wanakopata mafunzo ya kidini.
Kufanya hivi sio kuingilia na kukiuka uhuru wa kuabudu. Uadilifu ni muhimu katika kila sekta. Ili kuepuka watu wasio na habari kupotoshwa na wahubiri wenye misimamo mikali, vyama vya mashirika ya kidini vinapaswa kuwa msitari wa mbele kuhakikisha wanachama wao ni watu waadilifu kiroho ili wasiwe hatari kwa usalama wa taifa.
Kuna vyama kadhaa vya mashirika na madhehebu ya kidini na japo vinaweza kuwa na malengo tofauti, kupigana darubini kuhakikisha hakuna mhubiri, dhehebu au shirika linalopotosha umma kunafaa kutiliwa mkazo. Vyama hivi vikiwajibika, vinaweza kutoa habari za mapema mmoja wa wanachama akionyesha dalili za kupotosha wafuasi wake kupitia mafunzo hatari ya kiroho.
Uhuru wa kuabudu ambao Wakenya wamehakikishiwa na Katiba haufai kutumiwa kuwaua au kuwanyima haki zingine zinazowahakikisha afya ya mwili na akili. Kwamba baadhi ya mili iliyofukuliwa msituni Shakahola ni ya watoto wasio na hatia ni thibitisho kuwa mafunzo yaliyopelekea kifo chao, ni hatari kwa vizazi vijavyo na hivyo basi tishio kwa usalama wa taifa.
Uchunguzi ukikamilika na kilichosababisha vifo vya watu hao kubainika kikamilfu, wadau wote katika masuala ya kidini na kiroho, usalama na ustawi wa jamii na usalama, wanafaa kuleta vichwa vyao pamoja kuzuia maafa kama hayo. Kila raia ana uhuru wa kuabudu lakini serikali ina haki ya kulinda maisha ya watu ikiwemo dhidi ya mafunzo yenye itikadi kali.