MNAMO Oktoba 13, 2021, Rais Uhuru Kenyatta alikariri kuwa hatakubali hata inchi moja ya himaya ya Kenya kutwaliwa au kudhibitiwa na nchi jirani.
Alitoa kauli hiyo kwenye taarifa ya kukatalia mbali uamuzi wa Mahakama ya Kimataifa kuhusu Haki (ICJ) uliopendelea Somalia katika mzozo kati yake na Kenya kuhusu eneo la mpaka katika Bahari Hindi.
Lakini Rais asisahau alitoa kauli sawa na hii kuhusu mzozo wa Kenya na Uganda kuhusu umiliki wa kisiwa cha Migingo Ziwani Victoria.
Wiki jana, kwa mara nyingine, wavuvi ambao ni raia wa Kenya walikamatwa na maafisa wa usalama wa Uganda katika kisiwa hiki na kusafirishwa hadi nchi hiyo jirani ambako walilazimishwa kula samaki wabichi.
Ikiwa Migingo iko ndani ya Kenya, mbona Rais Kenyatta anaruhusu Wakenya kuhangaishwa na walinda usalama wa Uganda?