MNAMO Desemba 16, 2022 Bunge la Kaunti ya Nairobi lilimtaka Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja kuwaondoa watoto wanaorandaranda barabarani maarufu kama chokoraa na familia zinazoishi katikati mwa jiji.
Madiwani wa Nairobi walipitisha hoja iliyodhaminiwa na Naibu Kiongozi wa Wachache Esther Chege ambapo walimpa huyo makataa ya mwezi mmoja kuwaondoa watu hao katikati mwa jijini na kuwapelea katika vituo vya kurekebisha tabia.
Viongozi hao wamemtaka Gavana Sakaja kuharakisha ujenzi wa Kituo cha Kuwatunza Chokoraa katika eneo la Ruai kinacholenga kuhudumia jumla ya watoto 3,000 kwa wakati mmoja.
Gavana huyo wa Nairobi na madiwani wasije wakasahau kuwa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Huduma za Jiji la Nairobi (NMS) iliyovunjwa, Luteni Jenerali Mohamed Badi 2019 aliahidi kuwapelekea chokoraa hao katika vituo kama vile Bahati Reception Centre, Pumwani Reception Centre, Joseph Kangethe Reception Centre na hata Shirika la Vijana kwa Huduma za Taifa (NYS).
Kwa hivyo, badala ya kusubiri kukamilishwa kwa ujenzi kituo cha Ruai ambacho ujenzi wake haujulikani ikiwa utakamilika hivi karibuni, Gavana Sakaja anaweza kutumia vituo vilivyotambuliwa na NMS, kuwahamishia chokoraa hao.