NA WANDERI KAMAU
RIPOTI iliyotolewa majuzi kuhusu kiwango cha ukosefu wa ajira miongoni mwa watu waliohitimu chuo kikuu nchini, inapaswa kutufungua macho kuhusu mikakati tunayostahili kuweka ili kutatua tatizo hilo kabla halijageuka kuwa janga la kitaifa.
Kwa mujibu wa mawasilisho yaliyotolewa kwenye Kikao Maalum cha Mageuzi kuhusu Elimu, kilichofanyika wiki jana mtaani Karen, Nairobi, Kenya ni miongoni mwa nchi zinazoendelea kushuhudia idadi ya juu zaidi ya mahafala ambao hawana ajira.
Kenya iliorodheshwa katika nafasi ya 90 kati ya mataifa 193 kote duniani, miongoni mwa nchi zinazokabiliwa na idadi kubwa ya mahafala wasio na kazi.
Hali inayotonesha zaidi janga ambalo limekumba taifa kwa miaka kadha sasa la ukosefu wa ajira kwa vijana, hususan waliosoma.Kinaya ni kuwa, idadi kubwa ya vijana wanaomaliza masomo yao na kujiunga na taasisi za kiufundi wamepiga hatua kubwa kuliko mahafala wengi.
Ripoti ilieleza kuwa kwa wastani, mwanafunzi aliyemaliza chuo kikuu huchukua hadi miaka mitano kupata kazi nzuri.
Kwa upande mwingine, vijana waliomaliza kozi za kiufundi wanaanza kazi zao mara moja wanapomaliza mafunzo.
Inamaanisha kuwa kwa miaka mitano ambayo mwanafunzi aliyemaliza chuo kikuu atakuwa akitafuta kazi, kijana wa mafunzo ya kiufundi atakuwa amejijenga kimaisha.Ni wakati wadau husika na wanafunzi wenyewe kubadilisha mtazamo wao kuhusu taaluma za kiufundi.
Mabadiliko ya dhana ni miongoni mwa masuala makuu yanayofaa kuzingatiwa na jopokazi maalum lililobuniwa na Rais William Ruto kutathmini Mfumo wa Elimu ya Umilisi na Utendaji (CBC).
Lazima tutathmini upya taaluma zinazofunzwa katika vyuo vikuu vya humu nchini ili kutatua mkwamo huo.
Subscribe our newsletter to stay updated