NA WANDERI KAMAU
MWANADAMU ana mazoea ya kujikweza.
Huwa anapenda sana kusifiwa na kuenziwa hata kwa vitendo ama mafanikio ambayo hakuyafikia yeye mwenyewe.
Ni kutokana na mtindo huo ambapo utampata kiongozi wa eneo au jamii fulani akijifananisha na “mungu” wa watu anaowaongoza.
Mtindo huo ndio umewafanya watu wengi maarufu kuwa na mazoea ya kujikweza kwa kila namna, wakijipa tambuzi ambazo haziwafai hata kidogo.
Kwa mfano, katika nyakati tunazoishi, ni vigumu kumtambua “Daktari” ama “Profesa” halisi; maanake kila mmoja amejikweza kuwa mtu wa hadhi na kiwango hicho.
Kimsingi, profesa ni mtu anayeelewa ugumu wa safari ya usomi kutoka chini hadi kufikia kiwango cha kupata shahada ya uzamifu (PhD).
Hivyo, ni mtu aliyepitia katika shule ya msingi, sekondari na hatimaye chuo au vyuo vikuu kadhaa ili kupata shahada zake. Ni safari ndefu na ngumu sana.
Mbali na hayo, kabla ya kuwa profesa, huwa kuna hatua kadhaa za kiusomi ambazo mtu hupitia ili kufikia hadhi hiyo. Baadhi ya hatua hizo ni kwa daktari. Katika ulingo wa kiakademia, mtu hutawazwa profesa kulingana na mchango wake katika taaluma aliyosomea. Ni hatua ambayo wakati mwingine huchukua hata miongo kadhaa.
Hivyo, inashtua wakati mtu ambaye hajawahi kuingia darasani wala kujua uchungu wa safari ya usomi anajikweza hadhi kwa kujiita “Daktari” ama “Profesa” bila hata kujua undani wa maana na matarajio yatokanayo na utambulisho kama huo.
Wale ambao wamebuni mtindo huo ni viongozi wa kidini na wanasiasa. Kwa sasa, karibu kila mtu anayeongoza kanisa lake—kwa kuzingatia ukubwa wa ufuasi—ni ‘Askofu’, ‘Daktari’, ‘Nabii’ ama ‘Mtume.’
Ni muhimu kutaja kuwa makala haya hayaingilii viongozi ama madhehebu ya kidini kwa namna yoyote ile.
Hata hivyo, viongozi hao wanaipotosha jamii wanapojivika tambuzi zisizowafaa hata kidogo.
Kulingana na mafundisho ya kidini, askofu ni kiongozi anayeheshimika sana baada ya kupitia taratibu kali za kidini ili kufikia upeo huo. Ni neno lenye umuhimu mkubwa pia katika Kanisa Katoliki, kwani linarejelea kiongozi wa dayosisi inayojumuisha makanisa kadhaa.
Hivyo, matumizi yake katika madhehebu kongwe huwa yenye uzito sana. Mdahalo huu uliibuliwa na Profesa Njoki Wamae wa Chuo cha United States International University-Africa (USIU-A), aliyeghadhabishwa na watu wenye mazoea ya kujipa tambuzi zisizofaa, bila kujua safari ngumu ya kuzipata.
Ni kauli nzito, inayopaswa kuzindua taasisi kama Tume ya Kusimamia Elimu ya Vyuo Vikuu (CUE) kuweka taratibu kali kuwaadhibu wale wanaotumia tambuzi kama hizo isivyofaa. Wanakosea heshima wanaopitia taratibu zote kufikia kiwango cha kupewa tambuzi hizo.
Subscribe our newsletter to stay updated