Na MASHIRIKA
MABAO matatu ya kipindi cha kwanza yalisaidia Atletico Madrid kuwakomoa Real Valladolid 3-0 katika Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) mnamo Jumamosi na kusalia ndani ya mduara wa nne-bora jedwalini.
Alvaro Morata, Antoine Griezmann na Mario Hermoso walicheka na nyavu za Valladolid na kuchochea kikosi hicho cha kocha Diego Simeone kuvuna ushindi huo muhimu uliopunguza pengo la alama kati yao na viongozi Barcelona hadi 10.
Kufikia sasa, Atletico wanajivunia pointi 31, saba nyuma ya mabingwa watetezi Real Madrid na Real Sociedad wanaoshikilia nafasi ya pili na tatu mtawalia.
Ushindi dhidi ya Valladolid ulikuwa wa pili kwa masogora wa Simeone kusajili kutokana na mechi saba. Mkufunzi huyo raia wa Argentina alitumia mechi hiyo ya Jumamosi kumwajibisha fowadi Memphis Depay kwa mara ya kwanza tangu akatize uhusiano na Barcelona.
Sociedad waliendeleza presha kwa Real na Barcelona kileleni mwa jedwali baada kutandika Rayo Vallecano 2-0 katika mechi nyingine ya Jumamosi.
Ushindi wa Sociedad ulikuwa wa tano mfululizo katika La Liga na wa tisa mfululizo katika mashindano yote. Ushindi wa Atletico ulitokana na mabao matatu yaliyofungwa chini ya dakika 10 za kipindi cha kwanza.
MATOKEO YA LA LIGA (Jumamosi):
Atletico 3-0 Valladolid
Vallecano 0-2 Sociedad
Espanyol 1-0 Real Betis
Sevilla 1-0 Cadiz
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO