NA MASHIRIKA
TURIN, ITALIA
MARIO Balotelli huenda atafahamu hivi karibuni ikiwa atapewa namba na kocha Roberto Mancini katika mechi ya kufuzu kwa Kombe la Dunia 2022 kati ya Italia na Macedonia ya Kaskazini mwezi Machi.
‘Super’ Mario alijumuishwa na Mancini katika kikosi cha Azzurri cha wachezaji 35 Jumatatu kwa kambi maalum ya mazoezi mnamo Januari 26-28 ili kuona iwapo anaweza kurejea kusaidia Italia kuimarisha idara ya kufunga mabao ambayo haijaridhisha.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Inter Milan, Manchester City, AC Milan na Liverpool ameng’ara katika klabu yake mpya ya Adana Demirspor inayokamata nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu ya Uturuki.
Balotelli, 31, alijumuishwa katika kikosi cha Italia mara ya mwisho mnamo Mei 2018.
Kujumuishwa kwake kambini mwa Azzurri kumezua mjadali mkali Italia, hasa kwa sababu ya utundu wake katika klabu na timu ya taifa.
Ikifanikiwa kupiga Macedonia ya Kaskazini, Italia itamenyana na mshindi kati ya Ureno na Uturuki katika kivumbi cha kuelekea Qatar.