• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 9:55 AM
Bayer Leverkusen yapepeta Celtic bila haya katika Europa League

Bayer Leverkusen yapepeta Celtic bila haya katika Europa League

Na MASHIRIKA

MWANZO mzuri wa Celtic katika mchuano wa Europa League dhidi ya Bayer Leverkusen ya Ujerumani ulifumuliwa na masihara ya mabeki wao walioruhusu wageni kuwaponda 4-0 katika mechi iliyowakutanisha usiku wa Alhamisi jijini Glasgow.

Makosa ya David Turnbull yalimpa fowadi Piero Hincapie fursa ya kuwafungulia Leverkusen ukurasa wa mabao katika dakika ya 25 kabla ya Florian Wirtz kufunga la pili baada ya kumwacha hoi kipa Joe Hart kunako dakika ya 35.

Ingawa Celtic walipania kurejea mchezoni katika kipindi cha pili, makali yao yalizimwa kirahisi na Lucas Hilario aliyefunga penalti katika dakika ya 58 kabla ya Amine Adli aliyetoka benchi katika kipindi cha pili kuzamisha kabisa chombo cha Celtic mwishoni mwa mchuano huo.

Kichapo kinawasaza Celtic mkiani mwa Kundi G bila alama yoyote na kwa sasa wanajiandaa kumenyana na Ferencvaros ambao pia hawajashinda mchuano wowote kufikia sasa.

Leverkusen na Real Betis wanajivunia rekodi ya kushinda mechi zao mbili za ufunguzi wa Kundi G. Celtic walitumia mchuano huo dhidi ya Leverkusen kama jukwaa mwafaka la kuwakaribisha kikosini wanasoka Kyogo Furuhashi na nahodha Callum McGregor ambao wamekuwa nje kwa kipindi kirefu kuuguza majeraha.

Leverkusen walishuka dimbani kwa ajili ya mechi hiyo wakipigiwa upatu wa kuibuka ushindi ikizingatiwa kwamba wamepoteza mechi moja pekee kufikia sasa muhula huu – kichapo cha 4-3 dhidi ya Borussia Dortmund katika Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Leverkusen hawajawahi kusajili sare katika mchuano wowote kati ya 21 iliyopita katika soka ya bara Ulaya. Kikosi hicho kimeshinda mara 13 na kupoteza mechi nane kati ya hizo.

Mechi dhidi ya Leverkusen ilikuwa ya kwanza kwa Celtic kutofunga bao katika mashindano ya bara Ulaya tangu Disemba 2019 walipopigwa 2-0 na CFR Cluj katika Europa League.

  • Tags

You can share this post!

Sturridge apata hifadhi katika kikosi cha Perth Glory...

Shahidi apiga wakili ngumi kortini kwa kumuuliza swali