• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 10:44 AM
Bayern Munich wamsajili beki Omar Richards kutoka Reading FC

Bayern Munich wamsajili beki Omar Richards kutoka Reading FC

Na MASHIRIKA

BAYERN Munich wamemsajili beki wa kushoto wa Reading, Omar Richards, 23, kwa mkataba wa miaka minne utakaotamatika rasmi mnamo 2025.

Sogora huyo raia wa Uingereza alijiunga na akademia ya Reading mnamo 2014 na akaanza kuchezea kikosi cha kwanza mnamo Agosti 2017. Kufikia sasa, amewajibishwa na klabu ya Ligi ya Daraja la Kwanza nchini Uingereza (Championship) mara 106.

Kutua kwake kambini mwa Bayern kunatarajiwa kutoa ushindani mkali kwa beki Alphonso Davies ambaye amekuwa tegemeo kuu la Bayern kwenye safu ya kushoto uwanjani.

Mabeki David Alaba wa Austria na Jerome Boateng wa Ujerumani tayari wameagana na Bayern ambao ni mabingwa mara sita wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) baada ya kuongoza kikosi hicho kutia kapuni taji la tisa mfululizo la Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Bayern ambao kwa sasa watakuwa chini ya kocha Julian Nageslmann baada ya kuondoka kwa Hansi Flick, wamemsajili pia beki Dayot Upamacano kutoka RB Leipzig.

Richards atakuwa akivalia jezi nambari tatu mgongoni akiwa kambini mwa Bayern na anaungana na chipukizi wengine raia wa Uingereza ambao wameibukia kuwa masogora wa haiba kubwa duniani baada ya kuanza kucheza soka ya Bundesliga.

Hao ni pamoja na Jadon Sancho na Jude Bellingham wa Borussia Dortmund ambao tayari wameteuliwa na kocha Gareth Southgate kuwa sehemu ya kikosi atakachokitegemea kwenye fainali zijazo za Euro kati ya Juni 11 na Julai 11.

Fowadi wa zamani wa Leicester City, Demarai Gray pia alijiunga na Bayer Leverkusen mnamo Januari 2021 huku aliyekuwa chipukizi wa West Ham United, Reece Oxford akitia mkataba wa kudumu kambini mwa Augsburg mnamo 2019 baada ya kuchezea Borussia Monchengladbach kwa mkopo.

RB Leipzig walimsajili Ademola Lookman kutoka Everton mnamo Julai 2019 baada ya kuhudumia Fulham kwa mkopo. Kinda wa zamani wa Everton, Antony Evans pia anachezea Paderborn ya Ujerumani baada ya kusakatia Crewe Alexandra kwa mkopo.

Mnamo 2019-20, beki Nat Phillips wa Liverpool alichezea Stuttgart kwa mkopo huku beki Jonjoe Kenny akiondoka Everton na kutua kambini mwa Schalke.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Luka Modric atia saini kandarasi mpya ya mwaka mmoja...

Dkt Amoth ateuliwa kuwa makamu wa rais wa bodi tekelezi WHO