• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Beki Thiago Silva arefusha mkataba wake kambini mwa Chelsea kwa mwaka mmoja zaidi

Beki Thiago Silva arefusha mkataba wake kambini mwa Chelsea kwa mwaka mmoja zaidi

Na MASHIRIKA

DIFENDA Thiago Silva ameafikiana na Chelsea kurefusha mkataba wake uwanjani Stamford Bridge kwa mwaka mmoja zaidi.

Sogora huyo raia wa Brazil mwenye umri wa miaka 36, aliingia katika sajili rasmi ya Chelsea mwishoni mwa msimu wa 2019-20 baada ya kuhudumu kambini mwa Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa kwa kipindi cha miaka minane.

Uzoefu wake kwenye safu ya ulinzi umekuwa kiini cha uthabiti wa ngome ya Chelsea wanaojivunia ufufuo mkubwa wa makali yao chini ya kocha mpya Thomas Tuchel aliyemrithi Frank Lampard mnamo Januari 2021.

Silva aliwajibishwa kwa dakika 90 katika mchuano wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) ulioshuhudia Chelsea wakiwakung’uta Leicester City 2-1 mnamo Jumanne usiku ugani Stamford Bridge.

Tuchel ambaye ni kocha wa zamani wa Borussia Dortmund na PSG, amesema kuwepo kwa Silva kambini mwake kumeimarisha zaidi safu ya nyuma ya kikosi hicho ambacho kimefungwa jumla ya mabao 34 pekee kutokana na mechi 37 zilizopita ligini msimu huu.

Mnamo 2019-20, Chelsea waliokota kimiani mwao idadi kubwa zaidi ya mabao (54) miongoni mwa vikosi vilivyokamilisha kampeni za EPL katika orodha ya 10-bora jedwalini.

Hadi alipotua Chelsea, Silva ambaye amewajibishwa na timu ya taifa ya Brazil mara 94, alikuwa amevalia jezi za PSG zaidi ya mara 200 katika kipindi cha miaka minane na akanyanyulia miamba hao wa Ufaransa mataji saba mfululizo ya Ligi Kuu (Ligue 1).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO 

You can share this post!

ODONGO: Badala ya kupigia debe BBI, Raila afaa kuangazia...

WINNIE ONYANDO: Wazazi watafute muda kuwajenga watoto wao...