• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Borussia Dortmund wapunguzia Manchester United bei ya Jadon Sancho

Borussia Dortmund wapunguzia Manchester United bei ya Jadon Sancho

Na MASHIRIKA

BORUSSIA Dortmund wamewaeleza Manchester United kuweka mezani Sh11.4 bilioni ili wajitwalie huduma za kiungo chipukizi raia wa Uingereza, Jadon Sancho.

Iwapo Man-United watashawishika kufanya hivyo, basi watakuwa wameokoa Sh3.7 bilioni kutoka kwa Sh15.1 bilioni zilizokuwa zikidaiwa na Dortmund kwa ajili ya uhamisho wa sogora huyo mwenye umri wa miaka 21 mwishoni mwa msimu wa 2019-20.

Kufaulu kwa mpango huo wa kusajiliwa kwa Sancho kutamfanya mchezaji wa pili ghali zaidi kuwahi kutua Old Trafford baada ya kiungo Paul Pogba kusajiliwa na Man-United kwa kima cha Sh12.4 bilioni kutoka Juventus mnamo 2016.

Chini ya kocha Ole Gunnar Solskjaer ambaye ni raia wa Norway, Man-United waliweka mezani kima cha Sh11.2 bilioni ili kumshawishi beki na nahodha Harry Maguire kuagana na Leicester City miaka miwili iliyopita.

Huku Dortmund wakitaka fedha hizo kwa ajili ya mauzo ya Sancho kutolewa zote kwa pamoja, Man-United wangependelea kutoa malipo hayo kwa awamu mbili.

Dortmund wako radhi kumwachilia Sancho aondoke ugani Old Trafford ili wasalie na fowadi raia wa Norway, Erling Braut Halaand anayemezewa pia na Manchester City ambao wanatafuta mfumaji mrithi wa Sergio Aguero aliyeyoyomea Uhispania kuvalia jezi za Barcelona.

Licha ya kufuzu kwa kipute cha Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2021-22, Dortmund wana ulazima wa kuagana na baadhi ya wanasoka wao wa haiba kubwa msimu huu ili kupunguza gharama ya matumizi kutokana na athari za janga la corona.

Ili kuzamisha maazimio ya Man-City kuendelea kumfukuzia Haaland, Dortmund wamefichua kwamba bei mpya ya fowadi huyo wa zamani wa RB Salzburg nchini Austria ni Sh19.6 bilioni. Man-City waliokuwa waajiri wa zamani wa Sancho watatia kapuni bonasi ya Sh1.5 bilioni iwapo Sancho atafanikisha uhamisho wake hadi Man-United.

Sancho alianza kusakata soka ya kulipwa ugani Etihad na alikataa ofa mpya ya Sh4.2 milioni kwa wiki na kuhiari kuyoyomea Ujerumani akiwa na umri wa miaka 17. Hofu yake ilikuwa ni kukosa uhakika wa kuunga kikosi cha kwanza cha Man-City chini ya kocha Pep Guardiola aliyekuwa ametokea Bayern Munich wakati huo.

Kufikia sasa, Sancho amfungia Dortmund mabao 50 kutokana na jumla ya mechi 137. Anajivunia kufungia timu ya taifa ya Uingereza jumla ya mabao matatu kutokana na mechi 18.

Nyota huyo aliyezaliwa katika eneo la Camberwell, Kusini mwa jiji la London, alijiunga na akademia ya Watford akiwa na umri wa miaka saba kabla ya Man-City kumsajili kwa Sh9.2 milioni pekee akiwa na umri wa miaka 14. Uhamisho wake hadi Dortmund ulishuhudia Watford wakipokezwa na Man-City kima cha Sh70 milioni zaidi.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Waislamu Kenya gizani kuhusu kuhudhuria sherehe za hija

BURUDANI: Aamini yupo pazuri kutinga upeo wa kimataifa...