• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Cherotich, Wanyonyi wakata tiketi ya Riadha za Dunia U20 Colombia

Cherotich, Wanyonyi wakata tiketi ya Riadha za Dunia U20 Colombia

BERNARD ROTICH na AYUMBA AYODI

MAUREEN Cherotich (mita 5,000), Heristone Wanyonyi (kutembea kwa haraka 10,000m), Winnie Chepng’etich (kuruka umbali) na Peter Kithome (400m kuruka viunzi) mnamo Ijumaa walijikatia tikiti kushiriki Riadha za Dunia za chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20.

Wanne hao walishinda vitengo vyao katika siku ya kwanza ya mashindano ya kuchagua kikosi cha Kenya kitakachoelekea mjini Cali, Colombia mnamo Agosti 1-6 yanayoendelea uwanjani Nyayo.

Katika mashindano hayo ya siku mbili, ambayo yamevutia wanariadha 415 kutoka maeneo 14, Cherotich, ambaye alikuwa nambari sita kwenye Riadha za Dunia U20 jijini Nairobi mwaka jana, alisema alipata funzo na yuko tayari kuhakikisha anapata medali kwa kurekebisha makosa mjini Cali.

Cherotich alinyakua tiketi kwa dakika 15:14.26 akifuatiwa na Jane Gati (15:50.55) na Deborah Chemtai (16:10.01).

“Mbio zimekuwa nzuri na ushauri niliopata kutoka kwa kocha wangu zilinisaidia kufanya vyema. Nitaendelea kutia bidii mazoezini kwa sababu mashindano yatakuwa makali mjini Cali ambako tutakutana na wanariadha matata kutoka Ethiopia na Uganda,” alisema Cherotich kutoka shule ya upili ya Kalyet.

Wanyonyi aliachia wenzake vumbi katika kutembea haraka mita 10,000. Baada ya mizunguko 10 ya kwanza, alikuwa amefungua mwanya mkubwa. Alishinda kwa dakika 43:16.1 akifuatiwa na Stephen Ndakili (44:16.3) na Dominic Mwenda (45:50.0).

Wanyonyi, ambaye anatiwa makali na kocha Gabriel Otwane, hakumaliza kilomita 20 kwenye Riadha za Afrika nchini Mauritius zaidi ya wiki mbili zilizopita baada ya kupata jeraha. Mashindano ya kuchagua timu ya Kenya yatakamilika Julai 2.

TAFSIRI: GEOFFREY ANENE

  • Tags

You can share this post!

DOUGLAS MUTUA: Siri ya kuandaa uchaguzi huru ni kuheshimu...

Kenya Simbas wararua Uganda bila huruma Kombe la Afrika la...

T L