• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 1:15 PM
Everton wakung’uta Wolves katika EPL na kujiweka pazuri kunogesha Europa League msimu ujao

Everton wakung’uta Wolves katika EPL na kujiweka pazuri kunogesha Europa League msimu ujao

Na MASHIRIKA

EVERTON walidumisha uhai wa matumaini yao ya kunogesha soka ya Europa League msimu ujao baada ya kuwapiga Wolves 1-0 mnamo Jumatano usiku ugani Goodison Park.

Bao la pekee katika mchuano huo uliohudhuriwa na mashabiki 6,500 lilifumwa wavuni na fowadi raia wa Brazil, Richarlison Andrade katika dakika ya 48 baada ya kumtatiza kipa John Ruddy mara kadhaa.

Nusura Adama Traore awaweke Wolves kifua mbele katika kipindi cha kwanza ila juhudi zake zikazimwa na kipa Jordan Pickford aliyenyima pia Morgan Gibbs-White nafasi kadhaa za wazi.

Mbali na Richarlson, mwanasoka mwingine wa Everton aliyetatiza mabeki wa Wolves ni fowadi Dominic Calvert-Lewin. Everton kwa sasa wanashikilia nafasi ya nane kwenye msimamo wa jedwali la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa alama 59 sawa na nambari saba Tottenham Hotspur.

Masogora hao wa kocha Carlo Ancelotti waliingia ugani kumenyana na Wolves wakitawaliwa na kiu ya kujinyanyua baada ya Sheffield United kuwapiga 1-0 katika mchuano wa awali wa EPL uliowakutanisha ugani Goodison Park mnamo Mei 16, 2021.

Everton watafunga rasmi kampeni zao za EPL msimu huu dhidi ya mabingwa wa kipute hicho Manchester City mnamo Mei 23 uwanjani Etihad.

Hadi waliposhuka dimbani kuvaana na Everton, Wolves walikuwa wameshinda mechi moja pekee ya EPL kati ya 13 walizochezea ugenini. Klabu hiyo ya kocha Nuno Espirito Santo sasa inashikilia nafasi ya 12 kwa alama 45 na hii itakuwa mara yake ya kwanza kukamilisha kampeni za EPL nje ya orodha ya 10-bora tangu mwaka wa 2018. Wolves watakuwa wenyeji wa Manchester United katika mchuano wao ujao ugani Molineux.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

DIMBA MASHINANI: Kipa mahiri michumani kama mwanajeshi...

FWA yamtawaza beki Ruben Dias wa Manchester City Mchezaji...