• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Beki wa zamani wa Man-Utd, Patrice Evra, afichua aliwahi kudhulumiwa kimapenzi na mwalimu wake

Beki wa zamani wa Man-Utd, Patrice Evra, afichua aliwahi kudhulumiwa kimapenzi na mwalimu wake

Na MASHIRIKA

BEKI wa zamani wa Manchester United, Patrice Evra, amesema aliwahi kudhulumiwa kimapenzi na mwalimu wake alipokuwa tineja.

Mwanasoka huyo mwenye umri wa miaka 40 alifichua hayo mnamo Oktoba 22, 2021 kwenye mahojiano na gazeti la The Times, siku chache kabla ya kuzindua kitabu chake kipya.

“Sikutaka kufichua mambo yote awali. Nilikuwa na aibu ya kuzungumzia yaliyonisibu mikononi mwa mwalimu wangu wa shuleni. Niliogopa sana kusema chochote kwa sababu sikujua jinsi watu wangefikiria kunihusu,” akatanguliza.

“Sasa nina ujasiri wa kufichua yote kwa sababu nisingetaka mtoto yeyote apitie masaibu niliyoshuhudia,” akaendelea.

Evra, alikulia na kulelewa katika eneo la Les Ulis karibu na jiji la Paris, Ufaransa. Anasema mwalimu wake aliyekuwa akiishi naye katika nyumba yake alimdhulumu kimapenzi baada ya maamuzi ya kuishi naye kuafikiwa na mama mzazi aliyetaka kupunguza gharama ya Evra kusafiri mara kwa mara kwenda na kurudi shuleni.

Ingawa alimweleza mama yake kuhusu yaliyompata wiki mbili baadaye, mzazi alimkataza kabisa kufichua lolote wakati huo.

“Sasa nina umri wa miaka 40 na nina ukakamavu wa kusema kinachonihusu. Lililonisibu lilimkera sana mamangu. Lilimshtua pakubwa. Ilikuwa hadi majuzi tu alipoanza kulizungumzia jambo hilo peupe na hata kunikubalia kulitia kwenye kitabu changu. Alipinga sana mipango yangu hiyo hapo awali,” akaongeza Evra.

Katika kipindi cha miaka minane ya kuhudumu kwake ugani Old Trafford, Evra alisaidia Man-United kutia kapuni mataji matano ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Vikosi vyaweka rekodi mpya Uingereza kwa kuchanja penalti...

Mwanasheria mkuu kukata rufaa kuhusu uteuzi wa majaji

T L